NINGEWEZA kuiita nyumba ya ibada ya Kijiji. Kuiita kanisa si upendeleo wa kidini; la ni kutaka tu kuwa mwaminifu kwa yule niliyezungumza naye. Hivyo basi pale nitakapotaja Kanisa la Kijiji, wewe soma “Nyumba ya Ibada ya Kijiji” au “Hekalu la Kijiji” au “Msikiti wa Kijiji”.
Kwa hakika, unaweza kuita chochote kinacholenga kuwaunganisha watu wa kijiji, kitu kinachojenga umoja wa kijiji.
Mwaka 2006, kwenye jiji la Dar es Salaam, nilikutana na kijana kutoka Marekani. Kijana huyu aitwaye Ben Yanda, alikuwa akifanya utafiti kwenye Bonde la Rukwa. Yeye ni mfugaji, na utafiti wake ulielekea upande wa ufugaji. Si lengo la makala hii kuelezea mengi tuliyozungumza.
Kusema kweli nilizungumza mengi na kijana huyo; mfano alishangaa sana kukuta watu kule Rukwa, wenye uwezo wa kuuza zaidi ya ng’ombe 50 kila mwezi, na bado watu hao wanajiita masikini.
Aliushangaa utajiri mkubwa wa Watanzania wanaotembea kifua mbele wakiutangazia ulimwengu mzima kwamba wao ni masikini.
Baba yake huko kwao ni mfugaji, lakini hawezi kuota hata siku moja kuwa na ng’ombe zaidi ya 200 wakati kwenye Bonde la Rukwa kuna wafugaji wana ng’ombe zaidi ya 3,000. Hawa ni masikini? Hawa wanahitaji kusaidiwa? Hata hivyo, kwa nini wasaidiwe na wanasaidiwa na nani kwa msingi upi?
Kwa nini mtu kutoka Marekani, Ulaya, Japan au China awe na huruma kwa mtu wa Sumbawanga? Kwani wao kule Marekani hawana watu wa kusaidia? Kwa nini watusaidie? Kama wana upendo, kwa nini wasitoe nafasi ya masomo, vijana wetu wakaenda kusona na kurudi kuendeleza taifa letu?
Je, si kwamba wanatusaidia ili waweze kutunyonya vizuri? Si kwamba wanatusaidia ili watupumbaze tulale usingizi, ili watuibie vizuri? Kule nyuma walitutawala, walitununua kama samaki na kutupeleka utumwani – mapenzi ya kutusaidia yametoka wapi?
Ni mtu gani anaweza kusimama na kuelezea mapenzi ya ‘misaada’ kutoka nchi za nje? Ni nani anaweza kusimama na kuelezea ‘mapenzi’ ya makampuni ya kigeni kwa Tanzania?
Mfano mmoja ni makampuni ya simu yanayomnyonya maskini na tajiri? Viwango vya kununua muda wa kuongea vinalingana, tajiri na masikini wanalipa sawa. Kama wanatupenda, kwa nini wasitofautishe maskini na tajiri katika uwekezaji wao? Wanatupenda kutusaidia au wanatupumbaza watunyonye?
Hayo tuyaache, na tuangalie Kanisa la Kijiji. Kama kawaida yetu sisi tuliozoea kuwatenga watu katika makundi ya kidini; maana daima unataka kujua kama mtu ni Mkristu au Mwislamu. Kama wewe ni Mkristu, basi kasumba ni kwamba Mkristu ndiye ndugu yako wa karibu, na kama wewe ni Mwislamu, basi Mwislamu ndio ndugu yako wa karibu.
Lakini dhambi ya kuwatenga watu katika makundi, kama alivyosema Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere haishii hapo. Daima mtu utataka kujua kama mtu ni Mkatoliki, Mlutheri, Sabato nk. Au utataka kujua kama mtu ni Suni, Shia au dhehebu jingine la Kiislamu kama vile itikadi kali nk. Na kawaida yule wa dhehebu lako, ndiye unafikiri ni wa karibu zaidi. Dhambi inaendelea, maana daima utataka kujua kama mtu huyo ni mlei au ni wa daraja la kupakwa mafuta, na kama ni mlei na wewe ni mlei, basi unajisikia vizuri kwa mlei mwenzako, na kama ni mpakwa mafuta, na wewe ni mpakwa mafuta, basi utajisikia vizuri kwa mpakwa mafuta mwenzio.
Lakini dhambi inaendelea, maana utataka kujua kama ni padri au sista. Na kama ni padri, basi utataka kujua ni padri wa shirika gani na kama ni sista ni wa shirika gani. Mashirika mengine hayapikiki chungu kimoja!
Yako mashirika mengi ya kipadri, Majesuit, Wafranscano, Wabenedectin, Wakonsolata, Wakapuchin, Wa damu Azizi ya Yesu nk. Dhambi ya mgawanyiko inaweza kuendelea hadi kwenye umri, sura, kabila na wakati mwingine maeneo mtu anayoishi; wa Mbezi atamchukulia jirani yake kuwa ndugu wa karibu kuliko yule anayeishi Tabata na Ubungo!
Wale wanaoendesha magari ya kifahari wanajiona kuwa karibu zaidi. Na wale wa mkokoteni wanajiona wamoja zaidi ya wale wanaoendesha magari ya kifahari. Dhambi ya mgawanyiko inaendelea hadi kiasi cha kutisha.
Nilipokutana na huyu kijana Ben Yanda, kwa vile alionekana mcha Mungu, kwa kupenda kusali na kuongelea maadili ya kidini, nilitaka kujua yeye ni dini gani. Alikubali kwamba yeye ni Mkristu. Lakini kwangu hilo halikutosha. Nilitaka kujua ni Mkristu wa dhehebu gani na je ni padri, mchungaji, askofu au mlei.
Hapo ndipo maajabu yakaanza. Yeye hakuwa na habari ya dhehebu na wala hakuwa na ile kasumba ya kuwatenga watu katika makundi ya walei na wapakwa mafuta. Hakuwa na habari na cheo cha askofu! Alijua kundi la waumini wenye kiongozi wa ibada anayejulikana kama mchungaji. Na mchungaji huyu ni kiongozi wa ibada tu na wala si kiongozi wa kanisa, kanisa linaongozwa na waumini!
Alizaliwa akalikuta Kanisa la Kijiji! Kwa maneno mengine alizaliwa na kuikuta nyumba ya Ibada. Kwa maelezo yake ni kwamba, kijiji chao kina kanisa moja tu ambalo linaitwa Kanisa la Kijiji. Ni kanisa la kila mwanakijiji. Ni kanisa ambalo si la Kikatoliki, si la Kilutheri na wala si la
Sabato.
Ni kanisa ninalokumbatia kila mwanakijiji. Sharti la kujiunga na kanisa hilo ni kuwa mwanakijiji! Ni kanisa ambalo halina askofu wala uongozi wowote wa juu. Linaongozwa kwa ibada na mchungaji anayechanguliwa na wanakijiji na kuongozwa na kamati ya kijiji!
Ni tofauti na sisi tulivyozoea unalala na kuamka kukuta tangazo kutoka kwa Baba Mtakatifu kwamba fulani amechaguliwa kuwa askofu wa jimbo fulani. Ushiriki unakuwa mdogo, kazi zote anaachiwa Roho Mtakatifu anayevuma na kuleta ‘nguvu’ kwa wateule wachache!
Ben alisisitiza kwamba Kanisa la Kijiji, ni nafasi ya utakaso. Ni nafasi ya kuponya na kumtuliza kila mtu. Ni nafasi ya kufukuza upweke kwenye nyoyo za watu, nafasi ya kupigana na ubinafsi na kujenga moyo wa mshikamano wa kijiji kizima.
Kanisa la Kijiji ni kimbilio la kila mwanakijiji, ni maisha na moyo wa kila mwanakijiji. Ni kanisa lililoanzishwa na hitaji la wanakijiji wote – kulikuwa na hitaji ambalo hakukuwa na mtu wa kulipinga. Ni hitaji linalokuwa juu ya akili ya kila mtu, juu ya madaraka ya kila mtu na juu sifa ya kila mtu.
Kanisa la Kijiji ni nguzo ya maisha ya kila mwanakijiji. Kijiji kinasifiwa, kinatukuzwa na kupata heshima zote ambazo hakuna mtu wa kuzibinafsisha.
Kufuatana na maelezo ya Ben Yanda, ni kwamba kanisa hili la aina yake lilianza mnamo mwaka 1828, na limeendelea hadi leo hii. Kufuatana na maelezo ya Ben, kanisa hili ambalo halina mgawanyiko wa waumini limesaidia kwa kiasi kikubwa kujenga mshikamano na uzalendo mkubwa wa wanakijijini.
Kanisa limekuwa njia pekee ya kukutanisha watu wenye mawazo mbalimbali na kujadiliana kuhusu maendeleo ya kijiji chao. Maendeleo makubwa waliyonayo katika kijiji chao yanachangiwa kwa kiasi kikubwa na kuwa na nyumba ya ibada ya kijiji.
Nimearifiwa kwamba makanisa kama hayo ni mengi kule Marekani na yanatoa mchango wa aina yake katika jamii yao.
Kwa nini nilivutiwa na dhana ya Kanisa la Kijiji au Nyumba ya Ibada ya Kijiji? Nilipokutana na Ben, mjadala ulikuwa unapamba moto kuhusu Serikali ya Kikwete kwamba inawapendelea Waislamu.
Mjadala huu bado unaendelea. Ni mjadala ambao utaendelea siku zote; maana akitawala Mkristu, Waislamu wanalalamika kwamba Mkristu anawapendelea Wakristu. Akitawala Mwislamu, Wakristu wanalalamika, kama wanavyofanya sasa hivi kwamba kwa vile Kikwete ni Mwislamu, basi anapendelea Waislamu.
Tuligawanywa na wakoloni kwa ujio wa hizi dini za kigeni, na kwa vile tunafumba macho na kusinzia, tutaendelea kugawanyika hadi ujio mwingine wa wakoloni!
Baada ya kusikia habari hizo za Kanisa la Kijiji, nikawa na wazo kwamba labda na sisi hapa Tanzania tunahitaji nyumba za ibada za vijiji, kata, tarafa, wilaya, mikoa hadi taifa.
Tunahitaji nyumba za ibada ambazo hazikumbatii dini yoyote ile. Kama lilivyo Kanisa la Kijiji kule Marekani katika kijiji cha kijana Ben Yanda, ndivyo na sisi tunahitaji nyumba ya ibada isiyokuwa ya dhehebu wala dini.
Tunahitaji nyumba ya ibada isiyokuwa ya ukoo wala kabila. Tunahitaji nyumba ya ibada isiyokuwa na chama wala siasa. Nyumba ya ibada ya kuwakusanya Watanzania wote wa CCM, CUF, TLP, vyama vingine na wale wote wasiokuwa na vyama.
Tunahitaji nafasi ya utakaso, nafasi ya kuondoa kiburi na majivuno yasiyompendeza Mungu - majivuno ya elimu, majivuno ya pesa na utajiri, majivuno ya sura nzuri nk. Tunahitaji nafasi ya kuwakusanya wasomi na wale ambao si wasomi, nafasi ya kumnyenyekea kila mwanakijiji, kila mwana mkoa na kila Mtanzania.
Tumesikia maoni ya hekalu mara nyingi; kwamba kuna haja ya kuwa na Hekalu la Watanzania. Nimeandika mara nyingi juu ya hekalu. Wakati nikiwa na mawazo ya hekalu, nilikuwa sijafikiria juu ya Kanisa la Kijiji. Hata hivyo, sijachelewa ndo; maana leo hii nimeamua kuleta hoja hii ambayo ninaona ina umuhimu mkubwa katika jamii yetu ya Kitanzania.
Kanisa la Kijiji, ni mfano wa hekalu. Ni nafasi ya watu kusukumwa na uhuru wao wa ndani kujenga jamii yao. Kanisa la kijiji halisukumwi na siasa, halisukumwi na polisi, halina mahakama wala magereza. Ni utashi wa mtu kwa kusukumwa na imani ya rohoni ya kutaka kuhusiana na watu wengine. Ni utashi unaosukumwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe wa kutaka viumbe vyake viishi kwa mpangilio mzuri.
Kanisa la Kijiji ni chombo kizuri ambacho kinaweza kuwasaidia wanasiasa na serikali zote ziwe za demokrasia au za kidikteta.
Kama watu wamejipanga vizuri katika uzalendo wao na mapenzi yao kwa kijiji chao, kata yao, tarafa yao wilaya yao mkoa wao au taifa lao, inakuwa kazi nyepesi kuwaongoza na kuwaelekeza.
Binafsi nilivutiwa na Kanisa la Kijiji au nyumba ya ibada ya kijiji. Ninatamani kuanzisha moja, wewe una maoni gani?

Simu:
0754 633122