CCJ kisituondoe kwenye ajenda kuu
TOKEA kuanza kwa mchakato wa kukisajili Chama Cha Jamii (CCJ), kumekuwa na hisia mbalimbali kuhusu ujio wa chama hicho ambacho habari zake zinaendelea kupamba kurasa za magazeti mengi nchini.
Kumekuwa na mijadala ya kila aina kuhusu chama hicho ukiwemo ule unaohoji ni vigogo gani wa CCM wanaohusika na chama hicho. Mijadala hiyo ni kama vile hiyo ni mara ya kwanza kwa chama cha siasa kuanzishwa nchini.
Hivi kweli leo kuanzishwa kwa chama kipya cha kisiasa kuna ajabu gani wakati nchi yetu iliridhia kuwa na mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 na tayari tuna vyama vingi tu?
Hata baadhi ya viongozi wa chama tawala CCM wanaonekana kutaharuki na CCJ kana kwamba bado tumo kwenye ukiritimba wa chama kimoja.
Sisi tunasema kwamba kuanzishwa kwa CCJ kusitufanye Watanzania tuache kujadili masuala ya msingi ya nchi yetu, hasa yale yanayotukwaza katika maendeleo yetu.
Kwa mfano, Watanzania tunataka kujua hatima ya masuala ya ufisadi wa Kagoda Agriculture, Richmond, Meremeta na kadhalika. Ni muhimu tukajua hatima ya masuala hayo kabla ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Tunasisitiza kwamba CCJ, hata kama ni kweli kwamba huko tunakokwenda itabebwa na baadhi ya vigogo wa CCM, si hoja inayostahili kutuondoa katika ajenda yetu kuu ya sasa ambayo ni vita dhidi ya ufisadi.
Kwa hakika, hofu yetu kuu ni kwamba uanzishwaji wa chama hicho kipya na mjadala unaoendelezwa isivyo lazima wa ujio wake, kunaweza kukawa ni mbinu ya mafisadi au hata ya chama tawala CCM ya kufifisha skandali za ufisadi zinazoitetemesha nchi zikiwemo hizo za Kagoda, Meremeta, Kiwira na Richmond.
Tumalizie kwa kusisitiza kwamba CCJ ni chama cha siasa kama vilivyo vyama vingine vya siasa, na hata mchakato wa uanzishwaje wake hauna tofauti na tulioushuhudia kwa vyama vingine nchini wakati vilipoanzishwa.
Kwa maana hiyo, tusikubali kuondolewa katika ajenda ya msingi ambayo ni vita dhidi ya ufisadi. Kwa maana hiyo vilevile, tuendelee kuishinikiza Serikali hadi kieleweke kuhusu kashfa za Richmond, Kiwira, Meremeta na Kagoda kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
