Kwa Waziri wa Mikiki na Makeke,
Uzitoni Street,
Bongo.
Mpenzi Frank,
Waniuaua kipenzi waniuaua
Waniuaua kipenzi waniuaua
Nakuwazia kila saa waniuaua
Bila wewe sina raha waniuaua
Unasikia mpenzi? Na unasikia sauti yangu nyororo ikiimba huku macho yanakurembulia. Wacha wewe! Amini usiamini nakupenda sana. Sijui na hali yako ikoje wiki hii lakini mimi nimelegea kwa kukuwazia tu. Jitunze mpenzi wangu nikutuze.
Lakini mwaka huu sijui itakuwaje. Kama presha iko hivi mapema namna hii, kufika katikati ya mwaka itakuwaje. Itakuwa viharusi badala ya harusi. Nakuambia!
Sasa baada ya kuhimili presha ya kutangaza mali, imeingia presha ya nani yu chama kipya nani yu cha zamani. Watu wanavyonyoosheana vidole, lazima wengine watakuwa chongo tu. Na juu ya hapo, kuna mapambano ya uzee na ujana, wazee wawapishe vijana. Nakuambia mpenzi bosi anakonda hadi amelazimika kununua mkanda mpya suruali zisishuke ghafla.
Kwa mfano juzi, kaja jamaa, kavaa bonge ya suti. Baada ya kusalimiana, akaanza kumhoji kuhusu chama hiki kipya. Bosi akashangaa (au akajifanya kushangaashangaa maana wanasiasa Bwana ... akisema haendi kushoto, akiapa kwa miungu yote na mashetani juu haendi kushoto, utakuta kwamba kesho yake amemaliza kushoto kabisa).
‘Mimi? Nisaliti chama changu kipenzi? Samahani sana ndugu, wewe unanionaje? Hata siku moja.’
Jibu la bosi likanishangaza kidogo. Nikamwangalia huyu mgeni kwa jicho kali zaidi. Kweli sijawahi kumwona hata siku moja na bosi hakuonekana anamjua hata kidogo. Mwisho nikapata mawazo kwamba jamaa katumwa. Na kama katumwa basi ni kama bosi yuko mtegoni ndiyo maana anajibu hivyo.
‘Ni vizuri mheshimiwa. Tunajua uaminifu wako kwa chama. Lakini hawa wanaoitwa mafisadi unawaonaje?’
Bosi akaweka mkono moyoni na kuimba kama vile yuko kwenye ibada.
‘Ufisadi hauna nafasi katika chama chetu’
‘Hujajibu swali. Tunajua ufisadi hauna nafasi lakini wengine wamesema kwamba tumeruhusu mafisadi wapenye hadi kutawala chama chetu. Hapo unasema nini?’
Bosi aliangalia kushoto na kulia kama panya anayetafuta kujitoa mikononi mwa paka. Akajaribu kucheka.
‘Mbona maswali ya polisi ndugu yangu?’
‘Siyo maswali ya polisi lakini ni kipimo. Wewe ni mwenzetu au si mwenzetu? Mwenzetu atatetea kufa na kupona. Atakana ufisadi wa wenzake na kutukana wanaosema kuna mafisadi. Atakuwa tayari kuonekana mjinga kabisa ili mradi anashikana na kushikamana na wenzake wote. Mbele ya mashambulizi hakuna kudhoofika. Ni kusimama imara na wenzio. Unasikia?
Bosi alionekana kama mtoto mdogo kabisa.
‘Ndiyo mkuu. Mimi nawatetea. Nawatetea watu wote. Hawa wa nje hawajui jinsi sisi sote tunavyojitoa kwa faida ya nchi yetu.’
‘Sawa kabisa. Nimekuambia hivyo ujue kipimo cha sasa. Ni rahisi sana. Ama wewe ni mwandani mwenzetu au mwanje adui wetu. Hakuna kukaa katikati. Na tutakupima kwa maneno yako! Na watu utakaoambatana nao. Hii vita si lelemama.’
Mgeni akaondoka na bosi akakaa ameshika kichwa tu. Ghafla ikasikika hodi nyingine. Kufungua mlango, rafiki yake bosi. Bosi alifurahi sana.
‘Oh karibu rafiki yangu. Bora umekuja.’
Akamsimulia kidogo mazungumzo na huyu jamaa mwingine. Rafiki yake akacheka.
‘We Bwana unashangaashangaa nini? Hii ndiyo hali halisi. Mbele ya fununu ya chama kingine, tena fununu kwamba wao watameguka kutokana na hiki chama, lazima watabuni kila mbinu ya kubaki mbuni. Kila mtu sasa ni mtuhumiwa. ‘
‘Mtuhumiwa wa nini?’
‘Wa kuwasaliti na tabaka lao na ulaji wao. Kila neno unalolisema linachambuliwa sasa wapime msimamo wako. Na wanaamini kwa njia hii watashinda maana watu hawataondoka na wananchi wataendelea kusinzia usingizi wa pono.’
Bosi akauliza kwa wasiwasi kidogo.
‘Ina maana wote hawataondoka? Hiki chama kingine ni kiinimacho?’
‘Nadhani hii inategemea waheshimiwa kama wewe. Wakitangaza msimamo wao hakuna kiinimacho, wasipotangaza, na wananchi watarudi katika hali ya simanzi na huzuni. Tayari wamekata tamaa na wanasiasa, hii itakuwa ni uthibitisho wa mwisho kwamba hatuna wenye moyo.’
Bosi ghafla akapaza sauti.
‘Jamani hayo maisha siyawezi. Kwa nini nchi yetu haina wajasiri? Si wajasiriamali bali wajasirimsimamo. Kwani hatujui ni nani anayetajwa kujiunga na chama hiki?’
Mgeni akamkazia macho.
‘Mbona na wengine wanasema na wewe umo!’
Bosi akashtuka. Akaangalia kushoto na kulia.
‘Mimi? Ha ha mimi!’
.
‘Unaona sasa. Unawasema wengine na wewe je? Kwa nini kila mtu anamsubiri mwenzie awe jasiri kwanza? Nyinyi wote ni wasomi, mlikuwa na kazi zingine kabla ya kuingia kwenye siasa, mnaogopa nini? Kwani mtabaki mnaokota makopo?
Bosi akaangalia kushoto na kulia tena.
‘Kakuambia nani kwamba mimi ni mmojawao?’
Rafiki yake akatabasamu tu. Akaacha glasi yake ikiwa bado imejaa wiski nusu na kujiondokea. Alipofika mlangoni akageuka.
‘Sikiliza rafiki yangu, kama wewe ni Chama cha Wanene damudamu licha ya virusi zote zilizoingia kwenye damu na kusababisha magonjwa ya ufisadi, ya kiburi, ya upayukaji na kadhalika, ni vizuri. Labda wewe unaweza kupambana na virusi hivi vizuri kuliko hao wengine walioshindwa.
Naheshimu msimamo wako. Kama wewe pia una wasiwasi kwamba chama kingine kitakuja kuambukizwa na virusi vilevile kwa hiyo waona bora virusi ulizozoea, sawa pia, ingawa siheshimu sana msimamo huo.
Lakini kama unajua twahitaji chama kingine cha kupambana na virusi kwa namna tofauti na wasita kujiunga nacho kwa sababu umezoea maisha ya namna fulani, sikuheshimu hata kidogo. Waweza kuitwa mheshimiwa na dunia nzima lakini mimi najua kwamba hustahili heshima hiyo maana umetanguliza maslahi yako binafsi badala ya maslahi ya wananchi.’
‘Lakini mtoto wangu ...’
Mgeni akacheka.
‘Kwani nani hamjui mwanao? Msimamo mkali kama nini. Nasikia huko Ulaya baada ya vita kuu ya pili, watu waliokwepa kupambana na akina Hitler waliogopa sana kuulizwa na watoto wao ...’Baba ulifanya nini wakati wa vita?’ wasije wakaumbuka mbele ya watoto wao.’
‘Kwani unasema chama chetu ni cha mafashisti? Hili ni tusi rafiki yangu baada ya kazi yote tunayoifanya ... na kulinda hata uhuru wako wa kututukana.’
‘Usikwepe hoja. Utamjibu nini mwanao akikuuliza ...’wakati huu mgumu katika maendeleo ya taifa leto, ulifanya nini?’
‘Kumbe wewe umeshaingia kichwakichwa ...’
Mgeni akacheka na kuondoka na bosi akabaki ameinama.
‘Wapinzani, wapinzani kila mahali. Kwani sisi ni wabaya kiasi hicho? Na utamwamini nani akisema nini?’
Unasikia mpenzi, naona sasa hakuna nafasi ya mtu kubaki katikati. Ama kushoto ama kulia na wanaobaki katikati wanavutwa hadi makwapa yanaumia. Kweli mwaka huu tutaona mengi. Lakini mimi upande wangu nashangaa mambo mawili. Kwanza hiki chama cha wanene kinaogopa nini? Kinatamba kila siku kwamba kinapendwa na wananchi. Sasa kama kinapendwa kuna shida gani kikiundwa chama kingine? Kitapotea tu. Lakini kadiri wanavyohaha, tunapata picha nyingine.
Na pili kama alivyosema yule mgeni, hiki chama kipya hakitakuwa na maana kama tunawaona viongozi wake ni waoga, ni waoga kiasi kwamba hawako tayari kuthubutu, kupiga hatua bila kuwa na uhakika ili tupate chama chenye nguvu. Kama kweli wapo waliokereka na vitendo vya chama cha wanene, kadiri wanavyochelewa kuonyesha hivyo, watakiua chama hata kabla hakijazaliwa.
Au vipi mpenzi wangu
Mambo yote tisa ... isipokuwa kama kawaida yangu, sina haja na chama kingine, wewe ni chama changu na udumu ...tudumu humuhumu ndani ya mapenzi yetu
Hidaya wako.

Barua-pepe: