JENERALI Dwight Eisenhower wa Jeshi la Marekani, ambaye wakati wa Vita Kuu ya II ya Dunia aliongoza majeshi ya vikosi vya pamoja (allied forces) vya Ulaya, pia akipanga na kuongoza uvamizi dhidi ya Ufaransa na Ujerumani, mwaka 1944 hadi 1945, na baadaye mwaka 1951 kuwa kamanda mkuu wa Umoja wa Kujihami wa Nchi za Magharibi (NATO), anaamini uongozi ni busara, si mabavu licha ya kwamba ni jenerali. Anasema, uongozi si kukong’ota makonzi unaowaongoza.
Huyu ndiye aliyekuwa Rais wa 34 wa Marekani, mwaka 1953 hadi 1961, akiwa na rekodi ya kudhibiti shinikizo la Umoja wa Sovieti, enzi za vita baridi, lakini pia akiwa na rekodi ya kuwa Rais wa Marekani wa mwisho kuzaliwa katika karne ya 19 (alizaliwa Oktoba 14, mwaka 1890 na kufa Machi 28, mwaka 1969).
Kama nilivyoeleza, ingawa ni mwanajeshi -mpiganaji lakini haamini uongozi wa mabavu; bali busara na maarifa; vigezo ambavyo hatimaye huibua uamuzi sahihi, kwa wakati sahihi. Na kwa kawaida, bila shaka uamuzi sahihi kwa wakati sahihi, hufikiwa baada ya kupanga na kuchagua kwa usahihi.
Kigogo huyu mwenye rekodi za kishujaa katika medani za kijeshi, haamini kama kuongoza kwa kupiga watu makonzi ndiyo uongozi, bali ni unyanyasaji. Anasema; “You do not lead by hitting people over the head - that's assault, not leadership. Kwa upande wake, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere anasema; kupanga ni kuchagua. Je, viongozi wetu wanapanga na kuchagua bila kutugonga makonzi (kwa maana ya uamuzi kwa misingi ya uonevu)?
Je, wanapanga na kuchagua kwa usahihi, kwa vipaumbele sahihi na katika wakati sahihi? Tujadili maswali hayo kwa kutazama “aibu” ya Serikali kutenga Sh. bilioni 1.3 kama mgawo kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Augustine Ramadhani, kukarabati ( si kujenga nyumba mpya) makazi binafsi (sio ofisi).

Jaji Mkuu wa Tanzania, Augustine Ramadhani
Mjadala huu umekwishaanza, japokuwa umejikita kujadili tulipoangukia badala ya tulipojikwaa. Tahariri nyingi zimempongeza Jaji Mkuu, bila kuchambua chanzo cha tukio hilo; yaani watendaji (viongozi) ambao sasa wanathibitika kutokuwa na busara za kutosha. Hawajui waifanyie nini Tanzania na Watanzania.
Ingawa ni sahihi kumpongeza Jaji Mkuu kwa kutumia fedha hizo kujenga jengo la Mahakama ambalo ni kumbukumbu ya Jaji Mkuu wa kwanza mzalendo, Augustine Saidi, lakini kiini cha mjadala hakipaswi kuwa pongezi bali ni uamuzi wa viongozi (watendaji) serikalini kumega bilioni 1.3 kukarabati nyumba katika wakati usio sahihi (kiuchumi).
Waziri Mkuu Mizengo Pinda ndiye aliyefungua jengo hilo na kumpongeza Jaji Mkuu ambaye alilazimika kufichua siri kwamba fedha hizo zilipangwa kufanya kazi tofauti. Baadaye vyombo vya habari vilifuatia kwa pongezi. Lakini hatupaswi kupumbazika kwa pongezi za Waziri Mkuu au vyombo vya habari kwa urahisi kiasi hicho katika suala hili zito.
Tusipumbazike, tumuulize Waziri Mkuu, anamjua aliyeidhinisha matumizi hayo ya awali? Kama amemjua atamchukulia hatua gani au ataagiza mamlaka zilizo juu ya mhusika kumchukulia hatua? Au ndiyo yamekwisha hivi hivi?
Kama Waziri Mkuu bado hajamjua na wala hajishughulishi kumjua aliyeidhinisha makazi ya Jaji Mkuu kukarabatiwa kwa Sh. bilioni 1.3 (gharama zenye shaka mno), Watanzania wanataka kumjua kwa sababu amefanya uamuzi usio sahihi, katika wakati usio sahihi na kwa nchi isiyo sahihi; nchi inayonadiwa na viongozi wa kitaifa (Rais, Makamu na Waziri Mkuu) kuwa ni masikini.
Kimsingi, hatupigi kelele ili kumjua tu mhusika; bali pia ifahamike kuwa tayari amepoteza sifa ya kuwa mtendaji au kiongozi serikalini. Kumjua, kumfukuza au kumpunguzia madaraka nayo pia haitoshi. Waziri Mkuu anastahili kutoa tamko kuzuia upuuzi mwingine kama huo kuendelea kufanywa serikalini na hata kubatilisha kama mchakato umeanza.
Inafahamika, kipaumbele cha bajeti ya sasa ni elimu, ikifuatiwa na miundombinu. Miundombinu inayokusudiwa hapa kama kipaumbele ni ile inayohusu umma moja kwa moja na si miundombinu binafsi (makazi) ya viongozi.
Tutafakari: Je, ilikuwa sahihi katika nchi yenye migogoro ya ufadhili kwa wanafunzi wa vyuo vikuu, uhaba wa huduma za jamii hasa vijijini (majengo ya mahakama), nchi yenye bajeti inayotegemea wafadhili miaka nenda miaka rudi ikatenga Sh bilioni 1.3 kukarabati nyumba ya kiongozi mmoja tu?
Tatizo kubwa zaidi kwangu si utengaji wa fedha hizo, bali ni wakati ambao fedha zimetengwa. Si wakati muafaka. Kutenga bilioni 1.3 kwa ajili ya ukarabati katika wakati huu usio sahihi ni ufujaji.
Kwa uchumi unaoendeshwa kwa misaada na mikopo ya kitaifa na kimataifa, huu si wakati muafaka kuelekeza mabilioni ili kuwaridhisha viongozi fulani, familia na wageni wao. Eti akija Jaji Mkuu wa Marekani, basi amtembelee Jaji Mkuu wa Tanzania katika nyumba inayofanana na mgeni huyo kule Washington! Ni ajabu na aibu kwa nchi masikini kuwa na fikra hizo.
Wakati huu ambao huduma za jamii zimeporomoka mfano uendeshaji wa Shirika la Reli Tanzania ambalo ndilo tegemeo la walalahoi, si wakati muafaka kusikia maslahi ya viongozi yakitangulia maslahi ya wananchi. Ni aibu.
Upuuzi huu wa kukarabati nyumba kwa bilioni 1.3 katika wakati usio muafaka kiuchumi, ni sawa na ununuzi wa ndege ya Rais kwa mabilioni ya kiwango cha kutia shaka. Ni upuuzi sawasawa na ununuzi wa rada kwa gharama iliyopindukia. Hakika kwa mara nyingine, sehemu ya viongozi wenye kufanya uamuzi serikali wanathibitisha kutojua Watanzania wanahitaji nini na kwa wakati gani.
Naamini waliojadili na kupitisha uamuzi huu wa kipuuzi na wenye maswali mengi kuliko majibu bado wako hai, hatulazimiki kufukua makaburi yao ili tuchunguze vichwa na bongo zao. Ni dhahiri hawafai kubaki katika ofisi za umma kwa kuwa hawajui umma unahitaji nini.
Hawajui Taifa linahitaji nini na hawataki kutafakari au kujiuliza. Wanachojua ni viongozi wanataka nini. Si wenzetu, fikra au busara zao hazina msaada kwa Watanzania wala Tanzania.
Kama hii ni serikali makini, ina Waziri Mkuu makini na Rais anayenadiwa kuwa msikivu tuelezwe nani waliodhinisha mpango huu wenye dalili zote za ulaji. Lakini kuelezwa ni sehemu ya tu ya matakwa yetu bali pia wahusika au mhusika achukuliwe hatua kama kweli tunalenga kujenga Tanzania mpya, Tanzania bora kiutawala.
Haitoshi hatua ya Waziri Mkuu kuishia kumpongeza tu Jaji Mkuu akishindwa kutueleza hatua za serikali katika kudhibiti hali hiyo kutokea tena (si kwa maana ya viongozi kutokarabatiwa nyumba, bali kutofuja fedha). Ni muhimu Waziri Mkuu akaeleza umma kuwa hali hiyo itadhibitiwa vipi.
Kuna uwezekano mkubwa wakati Waziri Mkuu akimpongeza Jaji Mkuu kwa kutumia fedha hizo kwa kazi yenye manufaa zaidi kuliko kukarabati nyumba anayoishi, mabilioni mengine ya fedha za umma yanatumika au yamepangwa kutumika kukarabati majumba mengine ya wakubwa.
Viongozi wamekuwa hodari kuhubiri umasikini wa Tanzania. Hodari wa kuendeleza utegemezi wa Taifa, wakizurura katika nchi zilizoendelea kuomba ili kuziba pengo la bajeti ya Taifa lakini wakati huo huo, wanataka kuishi sawa na Waziri Mkuu wa Japan, Rais wa Marekani, Spika wa Uingereza, Jaji Mkuu, Mwanasheria Mkuu au Waziri wa Serikali mojawapo Ulaya. Hawataki kuishi na kuongoza kama viongozi wa nchi masikini na watu masikini.
Tujiulize: Serikali inayoweza kutoa mgawo wa ukarabati wa nyumba ya Jaji Mkuu Sh. bilioni 1.3, lakini ikibabaika kuwekeza fedha za kutosha kwa watafiti vyuo vikuu au kutoa fedha kwa ajili ya kuimarisha usafiri wa Reli ya Kati, inastahili kuendelea kuwa na watumishi waliopo?
Leo, Jaji Mkuu ameiumbua Serikali kwa kuchagua kipaumbele kingine chenye mantiki zaidi (kujenga jengo la Mahakama badala ya makazi binafsi), vipi kuhusu viongozi waliomegewa bilioni za ukarabati wa nyumba (binafsi) na kukaa kimya? Fedha kiasi gani zinatafunwa kwa njia hii? Bila shaka kama taifa, tumetumbukia katika kupanga na kuchagua uwendawazimu badala ya busara. Waziri Mkuu, wenzako wanasahau hata vipaumbele mlivyojipangia?
Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika

Simu:
0787-643151