MIMI si mpenzi mkubwa wa muziki; lakini kila niusikiapo wimbo wa Fresh Jumbe kuhusu mazingira, nasononeka. “Mazingira yeetuu, tunayaharibuu, na dunia yeetuu inateketea”; ni wimbo ambao kila niusikiapo nashikwa na huzuni na kuzama kwenye fikra.
Niliukumbuka wimbo huo, majuzi, wakati nikiangalia, kwa uchungu mkubwa (kupitia TV), wanavijiji wa wilaya ya Bududa, nchini Uganda, wakifukua udongo kuopoa maiti za wenzao waliokufa kwa kufukiwa na udongo katika janga la maporomoko ya ardhi (landslide) lililoikumba nchi hiyo hivi karibuni.
Janga hilo lililokumba vijiji vitatu vya wilaya hiyo ya Uganda limesababisha vifo vya watu 350. Ni moja ya majanga mawili makubwa yaliyoikumba dunia katika kipindi cha wiki mbili. Jingine ni tetemeko la ardhi huko Chile ambako watu zaidi ya 795 walipoteza maisha.
Nikiri kwamba wakati nikiangalia kwenye TV tukio hilo la kusikitisha la Bududa, Uganda, hisia na fikra zangu zilielekea katika tukio kama hilo lililotokea nyumbani kwangu, Same Mashariki ambako watu 25 walipoteza maisha katika janga la maporomoko ya ardhi yaliyotokea katika kijiji cha Goha, Novemba, mwaka jana.
Yawezekanaje maporomoko mawili makubwa ya ardhi yanayofanana yatokee katika nchi mbili jirani katika kipindi kisichozidi miezi mitatu? Hili ni swali ambalo pengine linastahili kujibiwa na wanasayansi, lakini kwa nilichokiona Goha; jibu kwangu ni dhahiri – uharibifu wa mazingira.
Same Mashariki, kama ilivyo wilaya ya Bududa nchini Uganda, imeathirika mno kwa ukataji miti holela kwa ajili ya mbao na usakaji wa maeneo mapya ya kilimo.
Tabia hii imesababisha ardhi ya maeneo hayo kuwa uchi. Bila kuwepo mizizi ya miti au mimea yoyote ya kukamata udongo, inapotokea mvua kubwa ikanyesha na kulainisha udongo huo, landslide haiepukiki.
Kwa ufupi, japo tetemeko la ardhi linaweza kusababisha janga hilo; lakini chanzo kikubwa cha landslide ni uharibifu wa mazingira. Hivyo ndivyo ilivyotokea katika kijiji hicho cha mlimani cha Goha, na ndivyo pia ilivyotokea katika vijiji vile vitatu vya wilaya ya Bududa nchini Uganda.
Swali la kujiuliza, ni je; maeneo mengine ya milimani katika Tanzania ni salama kiasi gani? Maana; kama chanzo cha majanga hayo ni uteketezaji wa misitu, basi, vijiji vingi vya milimani katika Tanzania vimo hatarini!
Na ukizingatia kwamba ndani kabisa ya ardhi ya sayari yetu hii, hivi sasa, kunatokota na matetemeko ya ardhi yaweza kufumuka dakika yoyote (Mbeya ilionja kidogo moja hivi karibuni), ni dhahiri hatari iliyoko mbele yetu ni kubwa zaidi.
Ndugu zangu, ninachotaka tukikumbuke leo, ni kile kilichoimbwa na Fresh Jumbe: Mazingira yeetuu tumeyaharibuu, na dunia yeetuu inateketea!
Kwa hakika, naweza kuongezea kidogo katika wimbo huo wa Fresh Jumbe kwa kusema kwamba; sasa ni wakati wa kulipia gharama za makosa tuliyoyafanya ya kuiharibu sayari yetu. Mother nature amecharuka, na sasa ni payback time, na ndiyo maana kila kukicha ni majanga, majanga na majanga zaidi sehemu mbalimbali duniani!
Kama huamini kwamba mazingira yetu tumeyaharibu na dunia yetu inateketea, hebu angalia orodha hii fupi ya majanga makubwa yaliyoitikisa dunia katika miaka ya karibuni:
Tsunami (Desemba 26, 2004) - watu zaidi ya 169,752 walifariki katika nchi 11, Kimbunga Katrina (Agosti 2005) – watu zaidi ya 1,300 walipoteza maisha huko New Orleans, Marekani, Haiti (Februari 2010) – watu zaidi ya 270,000 walipoteza maisha katika tetemeko hilo na Chile (la karibuni) ambako zaidi ya watu 795 wamepoteza maisha.
Hapa nimetaja majanga makuu machache tu kama mfano. Ningeweza kutaja pia matetemeko ya ardhi huko China (2009), mafuriko huko India (2009), mafuriko huko Afrika Magharibi na Kusini mwa Afrika (2009), ukame Kaskazini mwa Tanzania na Kenya nk. Kote huko, maelfu ya watu walipoteza maisha yao.
Nisisitize tena; mazingira yetu tumeyaharibu, na sasa ni wakati wa kulipia makosa yetu hayo. Sasa dunia inaishi kwa wasiwasi mkubwa. Kama ni tetemeko la ardhi, watu hujiuliza; baada ya Haiti na Chile ni nchi gani itafuatia? Itakuwa Asia au Afrika? Kama ni majanga ya aina ya Tsunami au Katrina, watu wanajiuliza; yataibukia tena wapi safari hii? Ni Ulaya au Afrika? Vivyo hivyo kwa mafuriko, vimbunga, volcano, ukame, njaa nk.
Pamoja na kwamba binadamu amejitahidi na kujiendeleza kisayansi; kiasi cha hata kuweka kituo huko anga za juu kabisa cha uchunguzi wa mwenendo wa sayari yetu hii (International Space Centre), bado wanaanga walioko huko wameshindwa kututahadharisha mapema na ujio wa majanga haya, bado kituo hicho kimeshindwa kumsaidia binadamu kuelewa vyema nini kinaendelea ndani ya ardhi ya sayari yetu hii au ndani ya bahari zetu.
Kwa maana hiyo, majanga haya yataendelea kuikumba sayari yetu kwa kushtukiza, na hivyo kuwakuta binadamu hawajajiandaa kabisa. Ilikuwa hivyo kwenye Tsunami, ilikuwa hivyo Haiti na imekuwa hivyo majuzi huko Bududa, Uganda.
Mazingira yeetuu, tumeyaharibuu na dunia yeetuu inateketea! Katika kipindi cha miaka 100 iliyopita binadamu wamechoma mikaa mingi na kulijaza anga na hewa ya ukaa! Tumetengeneza viwanda vingi, magari mengi, ndege nyingi; ambavyo vyote vinachoma mafuta yanayotoa hewa ya ukaa ambayo imelijaza anga letu!
Kutokana na hewa hiyo kujaa angani na kujenga tabaka la aina yake, joto limeongezeka duniani – ni kama vile milango ya jehanamu imefunguliwa; maana majanga kibao yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi (climate change) yamekuwa yakitesa kila kona ya dunia.
Kwa sababu ya matendo yetu hayo, vina vya bahari vinaongezeka kwa kasi kwa sababu barafu zinayeyuka kwa kasi katika maeneo ya baridi kali ya Arctic nk, na zikiyeyuka maji yake yanaishia baharini. Visiwa vinazama kwa kasi ya kutisha (kama huamini tembelea kisiwa cha Maziwe huko Pangani, mkoani Tanga, ujionee).
Sambamba na kuongezeka kwa vina vya maji baharini na kuongezeka kwa joto, mvua sasa hazitabiriki duniani. Kwingine zinakuwa nyingi kupita kiasi na kusababisha mafuriko na kwingine unakuwa ni ukame kamambe unaosababisha baa la njaa na vifo vya mifugo na viumbehai wengine. Wataalamu wanasema viumbehai karibu 2,000 vitakuwa vimetowka kabisa katika uso wa dunia ifikapo mwaka 2,050.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa (UN) iliyotolewa Desemba 14, 2009 inaonyesha kuwa robo tatu ya vifo vilivyotokana na majanga kwa mwaka huo vilisababishwa na mabadiliko ya tabianchi. Yalitokea majanga 245 duniani na kati ya hayo 224 yamesababishwa na mabadiliko ya tabianchi.
Ndugu zangu; Mazingira yetu tunayaharibu kwa kasi, na dunia yetu inateketea. Bila kubadilisha mienendo yetu, hakika miaka si mingi sana nasi tutateketea kwenye uso wa sayari yetu.
Wanasayansi wanahisi zamani kulikuwa na uhai katika sayari ya Mars ambayo sasa ni vumbi tupu jekundu. Kama ndivyo; tujiulize: Viumbe waliokuwepo huko Mars waliteketeaje wote? Nahisi viliteketea vyote kama ambavyo nasi tutateketea wote katika sayari yetu hii kama tutaendelea na kasi hii ya kuharibu mazingira! Je, tufanye nini kujiokoa?
Wakati tukivuta subira mataifa makubwa yakubaliane viwango vipya vya kupunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa duniani, wengine hatuwezi kukaa tu bila kufanya lolote.
Na hapo ndipo ninapowakumbuka Wapare wenzangu wale wa Goha (Same Mashariki); maana kama wasingekuwa ni sehemu ya uharibifu wa msitu wa Shengena, ardhi ya vilima vyao isingekuwa uchi, na pengine landslide ile isingetokea!
Ni uharibifu huo huo wa mazingira ambao umesababisha baadhi ya maziwa yetu makubwa yaanze kutoweka. Nilitembelea Ziwa Jipe, Ziwa Babati, Bwawa la Nyumba ya Mungu na Ziwa Manyara, na nilichokiona huko kilinitisha!
Kwa hiyo, kwa Wapare wenzangu wa Same Mashariki, na kwa wengine wote Tanzania, moja ya njia za kujiokoa na majanga haya yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi, ni kupanda miti kama vichaa na kukomesha kabisa biashara haramu ya magogo katika maeneo yao; hata kama itabidi kuweka ulinzi wa sungusungu!
Miti inasaidia sana kupunguza hewa ya ukaa inayozalishwa ambayo ndiyo chanzo cha mabadiliko ya tabianchi yanayoleta majanga haya. Na sote tunajua kupanda miti hakuhitaji mfadhili wa nje.
Tusipobadilika na kufanya hivyo, basi, tuwe tayari kuyakabili majanga – moja baada ya jingine, tuwe tayari kuzikabili hasira za mother nature.
Tuwe tayari kuyakabili majanga makubwa ambayo yako njiani; kwa maana kwamba tuwekeze katika hilo. Serikali, kwa mfano, inapaswa kuiboresha Idara ya Hali ya Hewa kwa kuipa vifaa vya kisasa na kusomesha watumishi wake ili waweze kuvitumia vizuri kututahadharisha kuhusu majanga.
Naamini idara hii, hata baada ya kuiboresha, haitakuwa na uwezo wa kututabiria, kwa usahihi kabisa, ni lini na wapi tetemeko la ardhi litatokea nchini; lakini angalau inaweza kututabiria masuala ya mvua kubwa zinazoleta mafuriko.
Kwa hali ilivyo hivi sasa, idara hiyo haiaminiki kabisa kwa sababu uwezo wake ni wa chini mno. Wiki iliyopita, wakuu wa mikoa waliilalamikia idara hiyo mbele ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika kikao chao kilichofanyika Dodoma.
Mizengo Pinda naye aliungana na ma-RC kuilalamikia idara hiyo kuhusu utabiri wake usio sahihi. Tatizo letu ni kwamba kila mtu analalamika, hata watendaji nao wanalalamika. Kwa mfano, Waziri Mkuu Pinda ana uwezo wa kuiboresha idara hiyo, lakini naye analalamika kama wengine.
Najua jibu la mkato na rahisi ni kwamba fedha hakuna. Lakini je, mabilioni wanayoyatumia kila mwaka kununua magari ya kifahari ya serikali, kama yangepunguzwa yasingetosha kuinunulia idara hiyo vifaa vya kisasa?
Je, fedha zinazotafunwa tunazoziona kwenye ripoti za CAG kila mwaka, kama zingeokolewa zisingesaidia kuiboresha idara hiyo nyeti katika zama hizi ambapo majanga yamekuwa kibao?
Maandalizi mengine kwa Serikali ni pamoja na kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya majanga, na hata kuunda kikosi maalumu cha kukabiliana haraka na majanga pindi yanapotokea. Nazungumzia masuala ya uokoaji na ujenzi wa miundombinu au makazi yanapoharibiwa na majanga.
Hebu fikiria: Kama mpaka sasa Reli ya Kati imefungwa kwa sababu ya kukatika kwa daraja kulikotokea wakati wa mafuriko ya Kilosa ya Januari mwaka huu, hali ingekuwaje nchini kama mafuriko yale yangetokea pia sehemu nyingine nchini na kukata madaraja mengine (mfano daraja la Wami)?
Ukweli ni kwamba, serikali yetu bado imelala usingizi. Haijajiandaa kabisa kukabiliana na majanga makubwa yanayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi. Hata wimbo wa Fresh Jumbe umeshindwa kuiamsha usingizini! Mazingira yeetuu, tunayaharibuu na dunia yeetuu inateketea!
Tafakari.

Barua-pepe: