Ifuatayo ni sehemu ya pili na ya mwisho ya mahojiano ambayo mwandishi wetu, Godfrey Dilunga aliyafanya na kada wa siku nyingi wa CCM na waziri mwadilifu wa zamani nchini Paul Kimiti. Sehemu ya kwanza ya mahojiano hayo ilichapishwa toleo lililopita.
Raia Mwema: Ninyi viongozi mnaomjua Sokoine, kwa nini msiandike kitabu maalumu kuhusu uongozi wake na wenu ili kutoa fursa kwa vijana wa sasa kufahamu rekodi nzuri za viongozi wazalendo wa zamani?
Paul Kimiti: Tuko watatu tuliowahi kuwa naye ofisini. Yuko Mheshimiwa Anna Makinda, Gertrude Mongela na Mheshimiwa Jackson Makwetta.
Wapo wengine waliowahi kufanya naye kazini, lakini sisi tuliwahi kuwa wasaidizi wake wa karibu zaidi.
Yako mengi ambayo tunaweza kuandika, lakini nimeona vitabu vingi vimeanza kuandikwa juu yake.
Kwa kweli, wakati mwingine bila kufanya mkutano wa pamoja wakati mwingine kila mmoja anaweza kutoa hadithi za ajabu, hadi mkajikuta mnajichanganya wenyewe.
Sasa wakati mwingine tunangoja mpaka tunakaribia kustaafu au kustaafu ndiyo tunaweza kuandika maisha yangu ya uongozi wa nchi.
Raia Mwema: Katika uongozi wa Awamu ya Pili, binafsi ukiwa kiongozi wakati huo unakumbukumbu gani ya kujivunia?

Paul Kimiti
Paul Kimiti: Mzee Mwinyi, mwaka 1989, alinipa nishani ya utumishi bora akiwa Rais. Ninayo mpaka sasa.
Raia Mwema: Rais Mwinyi alikuwa na viongozi wengi wanaomsaidia. Nini hasa kilimvutia hadi kukupa nishati hiyo?
Paul Kimiti: Kilichomvutia ni utendaji wangu wa kazi na hasa nilipohamia Mbeya. Kwa sababu Mbeya nilikuta mji umeharibika sana, barabara zote zilikuwa mbovu.
Kipindi hicho hali ya uchumi haikuwa nzuri barabara zote za miji yote zilikuwa mbaya. Mimi nilitumia ujanja wa kukutana na wafanyabiashara na wananchi kuzungumza, mimi nikiwa mkuu wa mkoa.
Tukasema hali ya serikali kifedha siyo nzuri, na kutengeneza barabara ya lami haiwezekani, tukaulizana sisi tunaweza? Na kwa taarifa yako hawakuamini kama tutaweza.
Sasa nilichoanza kufanya nikazungumza na wafanyabiashara. Kitu gani kinahitajika kujenga lami, wakasema kwanza kokoto, pili; magari ya kusomba hizo kokote.
Tatu; upatikanaji wa lami yenyewe, nne; vifaa vya kujengea. Nikasema sawa. Nilichofanya nikawafuata Wachina ambao kwa wakati ule walikuwa na mtambo wao wa kusaga kokoto za TAZARA eneo linaloitwa Mswiswi, unapokwenda Mbeya kuna sehemu inaitwa hivyo. Ni eneo lenye kokoto nyingi sana.
Nikakutana nao nikawaomba, nikawaeleza jamani sina fedha lakini nataka kubadilisha mji wangu.
Raia Mwema: Kabla hujaendelea. Mpango huu ulikuwa ni ubunifu wako ukiwa mkuu wa mkoa na si maelekezo kutoka Serikali Kuu?
Paul Kimiti: Ndiyo, huko serikali kuu hawakuwa na habari hiyo. Nikawaomba Wachina wanisaidie kokoto, wakanielewa wakasema niwaambie kiasi chochote ninachohitaji watanipa, nikaridhika.
Lakini sasa tatizo la pili namna ya kubeba kokoto na ni umbali wa Kilomita 25 kutoka mjini. Nikaona nikutane na wafanyabiashara, tena nilikuwa nakutana nao nyumbani sio ofisini.
Nilikuwa nakutana nao nyumbani ili waone mimi ni mwenzao. Sasa nikawaambia kokoto ninazo, sina malori. Wakajitolea wakasema tunayo malori kama 30.
Lakini wakasema tutatoa malori hatuna mafuta. Nikakutana na wenye vituo vya mafuta, nikawaomba wajaze angalau kila lori full tank ya mafuta. Sikutaka fedha zao taslimu hata kidogo.
Kazi iliyobaki ilikuwa ni wapi naweza kupata lami. TPDC walikuwa na mapipa ya lami pale nje ya Stadium (Uwanja wa Mpira-Dar es Salaam), hawakuyatumia.
Sasa nikasema jamani naenda Dar es Salaam kuzungumza na watu wa TPDC, nikafika nikazungumza nao nikawaambia jamani lami mnayo kwa nini msiniazime…wakasema mzee ibebe tutalipa mbele ya safari.
Sasa namna ya kubeba lami kutoka Dar es Salaam hadi Mbeya siwezi, sina uwezo. Hivyo nikaomba malori yanayotoka Dar es Salaam kwenda Mbeya kuja kuchukua Tumbaku Chunya, nikaomba kila anayekuja anichukulie angalau pipa nne au tano.
Na wale wanaotuletea hata mbolea kila wanapokuja Mbeya kuleta mbolea watuletee pipa hizo nne au tano, basi nikashtukia tayari lami ipo na imefika Mbeya bila kutumia hata senti ya serikali.
Kazi iliyobaki ikawa ni machine au mitambo ya kufanyia hiyo kazi. Ikabidi nizungumze na kampuni inaitwa Partisan Support, ilikuwa inatengeneza lami kutoka Igawa kuelekea Songwe.
Nikakutana nao nikasema jamani mimi nina kila kitu mashine zenu naomba mniazime angalau Jumapili lakini nitakuwa nawalipa overtime wafanyakazi wenu.
Wakasema na sisi mchango wetu ni kukupa mashine ila wafanyakazi wape angalau Sh. 10,000 kila mmoja itawatosha. Kazi ikaanza bwana mdogo kama utani.
Ule mji ulibadilika watu hawakuamini hadi watu wa Benki ya Dunia walikuja kuniuliza umepata wapi fedha kwa ajili ya ujenzi huu mzuri wa barabara? Hawakuamini.
Nenda Mbeya sasa hivi kila mmoja anazungumza lami ya Mzee Kimiti. Ni utundu tu.
Raia Mwema: Kwa maelezo yako, ulikuwa kiongozi mwaminifu usio na chembe ya ufisadi. Je, ni kweli uaminifu wako ndiyo ulifanya wananchi washirikiane nawe kwa kiwango hicho?
Paul Kimiti: Ndiyo, sana. Huwezi kuamini hata sasa. Sasa baada ya kutengeneza barabara mjini tukaanza kazi nyingine. Nikaagiza wote wanaozunguka barabara waanze kupanda miti ili mji upendeze.
Halafu wale niliowatengenezea lami slabs zao zinazokwenda kwenye maduka nao waweke cement (saruji).
Mji ulipendeza sana. Kwenye barabara kuu inayokwenda mpaka Tunduma, pale nikaoimba serikali sasa kwenye mpango wao waweke zile tunazoita service roads (barabara za pembeni) kwa sababu barabara itakuwa so busy na watu watamalizwa kwa ajali.
Wakaona hilo wazo ni jipya lakini nikaishawishi serikali hadi ikakubali. Jambo hilo lilifanya wenzangu wa Mbeya waone kwa kweli kuna uongozi.
Lakini pia nilikuwa natembelea wilaya karibu zote kuhimiza mambo ya kilimo na shughuli nyingine zote.
Raia Mwema: Inaonekana unaamini katika dhana kwamba, maendeleo yanapaswa kuanzia kwa mtu na baadaye vitu. Katika Wizara ya Kazi, mambo gani makubwa umeyafanya?
Paul Kimiti: Kwanza tulianza kuangalia sera zetu za utumishi. Mojawapo ni sera ya wafanyakazi ambao ndiyo walikuwa chini ya wizara hiyo kwa hiyo tuliona ni lazima wawe an uhuru wa kuzungumza mambo yao na ruksa hiyo ianzie kwenye sera.
Katika kipindi changu mabadiliko hayo ndiyo yalianza kujitokeza, wafanyakazi waliweza kujipanga, kuanzisha vyama vyao huru zaidi.
Lakini ni kipindi ambacho tulianza kubadilisha hizi sera zinazohusiana na mafao ya wafanyakazi. Kwa mfano, NPF (National Provident Fund) kuja NSSF ilikuwa ni kipindi changu tukiwa na Mustafa Mkulo (Waziri wa sasa wa Fedha) ambaye alikuwa mtendaji mkuu wa NPF na baadaye NSSF.
Lakini pia tulitaka kufikia sehemu fulani tuwe na sheria na kanuni ambazo wafanyakazi hawatonewa. Na mimi nikwambie ukweli wafanyakazi wengi hawatanisahau.
Mfanyakazi yeyote aliyekuwa anaonewa nilihakikisha anapata haki yake. Awe kampuni ya binafsi au serikalini kama ameonewa nitamrudisha kazini.
Wakati mwingine watu wanaoneana kwa mambo madogo sana na mimi sikupenda, na hadi kampuni nyingine walikuwa wananiita Mr. Green.
Raia Mwema: Kwa nini walikupachika jina la Mr. Green?
Paul Kimiti: Waliniita hivyo kwa sababu mawaziri tunasaini vile vibali vya kumrudisha mtu kazini kwa kalamu yenye wino wa kijani. Sasa walikuwa wakishaona tu wanasema Mr Green anamrudisha mtu waliyetaka kumfukuza.
Baada ya hapo mwaka 2000 nikagombea na kufaulu na kwa taarifa yako wakati wote nikiwa nagombea kura zangu zilikuwa zikiongezeka.
Mwanzoni niliogopa nilipokosa uwaziri mwaka 2000 hadi 2005 nikadhani kura zangu zitaporomoka kwa sababu nimekosa uwaziri.
Lakini kote kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa iliyofuata ambayo ilikuwa 2002 sikuwa waziri lakini kura nilizopata zilikuwa kati ya watu 10 bora katika nafasi zile 20.
Na kwenye Bunge mwaka 2005 kura zilikuwa nyingi sana kuliko miaka mingine yoyote.
Raia Mwema: Je, unadhani kwa nini walikuamini licha ya kuondolewa kwenye uwaziri, kete ambayo ingeweza kukuangusha?
Paul Kimiti: Ni kweli hawakuwa wananichagua kipindi chote kwa sababu tu mimi ni waziri au kwa kwa kuwa nina cheo kingine. Hapana, walikuwa wananichagua mimi Kimiti na si madaraka ninayoingia nayo kwenye kura.
Niseme tu kwamba utu wako binafsi ndiyo utakaokufanya ufanikiwe, siyo cheo. Viongozi wanadanganyika, unajua cheo unaweza kuwa nacho na wakakuangusha kwenye uchaguzi.
Sasa utu ndiyo msingi wa mafanikio na hasa kwa upande wangu. Ndiyo maana nasema nguvu za mamba ziko kwenye maji na nguvu za viongozi ziko kwa watu.
Raia Mwema: Kuna maneno yanasemwa kwamba umewahi kupendekezwa na kuridhiwa na Rais Mkapa kuwa Waziri Mkuu wake mwaka 1995, lakini siri ikavuja na uteuzi ukafutwa. Ni kweli?
Paul Kimiti: Mimi pia nilikuwa nasikia, si mwaka 1995 tu hata mwaka 2000 na hata 2005 yakizungumzwa majina la Kimiti linatajwa, nikasema…utadhani waandishi wa habari wananifanyia kampeni.
Lakini mtu mmoja akaniambia hapana, waandishi wa habari hawawezi kukufanyia kampeni kwa hali hiyo, bali wanaangalia utendaji wako wa kazi. Wanaona kati ya viongozi waliopo na Kimiti yumo, anastahili.
Mwandishi wa habari hawezi gazeti lake akamwandika mtu wa ovyo ambaye jamii na wenzake watamshangaa hata huyu mnamwandika anastahili kuwa katika nafasi hii?
Hivyo kila mwandishi anajitahidi kuwa makini kwamba nikimtaja fulani wengi wataamini ni sahihi na inaweza kuwa hivyo. Kwa hiyo hayo unayosema yamesemwa na niliyasikia.
Raia Mwema: Ulipokuwa ukisikia haya yanaandikwa na kuzungumzwa, yalikunyima usingizi?
Paul Kimiti: Mimi nilikuwa wakati mwingine nilipata shida nikidhani kwamba wananichongea. Nilikuwa na wasiwasi wananichongea ili nionekane nafanya kampeni zangu mwenyewe ili waniandike.
Unajua kisaikolojia unakuwa mwoga kwamba wengine wanaweza kudhani kuwa nafanya kampeni kupitia kwa waandishi wa habari wakati hata mmoja sikuzungumza naye.
Lakini pia hata waandishi wasingeweza kuandika mtu ambaye tabia yake ni mbaya hata kama watapewa hela ngapi. Sasa bwana mdogo mimi nasema haya yametokea hujui Mwenyezi Mungu ndiye anayepanga yote hayo.
Mimi nimeridhika, nimekwishafanya kazi nyingi kwenye nchi hii.
Raia Mwema: Nilikuwapo kwenye msafara wa kampeni za Rais Kikwete 2005 katika Uwanja wa Nelson Mandela, Sumbawanga. Kikwete alikuita jukwaani na kuwaomba wananchi wakuchague ili akutumie. Je, amekwishakutumia kwa namna gani kiuongozi au umesahaulika?
Paul Kimiti: Nasema, nimetumika sehemu nyingi kwenye bodi mbalimbali kwa mfano Bodi ya Air-Tanzania nimekuwa mjumbe wa bodi, huwezi kuchaguliwa kuwa mjumbe wa bodi bila ‘wazee’ kuridhika.
Kwenye kamati mbalimbali nimekuwa kiongozi wa African Population Commission-African Union, si kazi ndogo. Kama tabia zako ni mbaya wenzako hawawezi hata kukufikiria kuwamo humo.
Kwa hiyo, leadership imekuwa karibu mno na mimi. Nimekuwa nikienda mikutano mingi sana Marekani, Sweden, China, Japan, kote nimekuwa nikienda kuiwakilisha serikali katika mikutano mbalimbali.
Hivyo bado, nadhani viongozi wangu wamekuwa wakinitumia kwa namna mbalimbali. Unajua wakati mwingine kukutumia si lazima wakupe cheo.
Anaweza kuona uzoefu ulionao, ukuu wa mikoa na uwaziri utatufaa kutuwakilisha katika mikutano mbalimbali. Namshukuru sana Mheshimiwa Kikwete ninapoona nateuliwa kwenda kwenye mikutano hii mbalimbali. Naona ni yeye mwenyewe anaridhia.
Raia Mwema: Hukuwahi kuhusishwa na ufisadi au rushwa. Wakati wa Mwalimu Nyerere utawala ulikuwa mkali tunaweza kusema labda uliogopa, lakini hata uongozi uliofuata ulibaki mtulivu. Umekwepa vipi mitego ya kukufikisha hapo?
Paul Kimiti: Ni tabia yangu binafsi, sipendi kujilimbikizia mali, sidhani kama kuna vitu vingine vya ziada nahitaji kama nalala na kula vizuri. Hilo la kwanza.
Pili, hawa wazee ambao nimekuwa nao kuanzia Mwalimu Nyerere na Sokoine hata na Mzee Mwinyi, ni wazee ambao hawakuwa na tamaa za ajabu ajabu. Haya ndiyo mambo ya msingi.
Raia Mwema: Hukuwahi kutumbukia katika kashfa za rushwa, lakini pengine umewahi kupata msukosuko na kujikwepesha dakika za mwisho. Tukio gani unakumbuka lililotaka kukutumbukiza kwenye kashfa hiyo?
Paul Kimiti: Ngoja nikwambie kitu ambacho kilinitisha kwa mara ya kwanza. Mwaka 1983 nikiwa Waziri ofisi ya Waziri Mkuu, nilianza kujenga nyumba hapa Dodoma.
Na nilijenga nyumba hapa Dodoma-Kilimani kwa mkopo wa Benki ya Nyumba (THB) nilipata mkopo wa 80,000 tu.
Lakini baada ya mwezi mmoja Mwalimu Nyerere akapata habari, akaniita akasema Paul nasikia unajenga nyumba umepata wapi hela?
Hilo peke yake inakufanya kuwa na hofu ya kufanya maovu, unaona kila mtu anakuona unachofanya. Sasa angekuwa hajaniuliza ningeweza kufanya mambo kimya kimya tu. Hili ni tukio lililonishtua.
Raia Mwema: Kulitokea nini baada ya Mwalimu Nyerere kukuita na kukuuliza hivyo?
Paul Kimiti: Aliponiuliza Paul umepata wapi hela, nikasema Mwalimu ni kweli najenga nyumba lakini hata kesho naweza kukuletea risiti zote. Nimepata mkopo kutoka THB (Tanzania Housing Bank) na ninakatwa kwenye mshahara wangu, nimeona ili nianze kuangalia namna ya kujenga maisha kwa ajili yangu na wanangu, niwajengee msingi hapa ni makao makuu ya nchi.
Siku moja baadaye nitashindwa hata kupata kiwanja hapa. Hakuna anayejenga, mimi ndiye waziri wa kwanza kujenga hapa Dodoma (kwa wakati huo) na umetaka tuanze kujenga hapa. Mwalimu kama nimefanya kosa nihurumie.
Akasema nashukuru sana una akili sana. Kumbe alikuwa anazo taarifa zote kuwa najenga kutokana na fedha za mkopo.
Raia Mwema: Kama alikuwa na taarifa unadhani kwa nini aliamua kukuita na kukuuliza?
Paul Kimiti: Nadhani ni kwa sababu watu walimpelekea maneno na inawezekana ya ukweli au kinyume chake kwa hiyo ikamlazimu anisikilize binafsi nasemaje.
Sasa akathibitisha kutoka kwangu. Kwa hiyo nikajua kuwa kila unachokifanya kuna watu wanaona na wanapeleka habari tofauti na siku hizi.
Siku hizi unaweza kujenga ghorofa na hakuna anayekuuliza wapi umepata hela.
Raia Mwema: Hii unadhani inatokana na nini, hili suala watu kufanya mambo bila uangalizi unaohakikisha kila linalofanyika linahifadhi maslahi ya nchi.
Paul Kimiti: Nadhani tumefikia mahali fulani uhuru wa kufanya mambo kwa ajili ya maendeleo binafsi tumeuacha wazi mno, hakuna mipaka rasmi.
Inawezekana viongozi wengi wamewekeza zaidi fikra zao katika maendeleo binafsi na baadaye ndiyo maendeleo ya Taifa, sitaki kusema hivyo moja kwa moja.
Wengine kweli wanaangalia zaidi familia zao kwamba kazi hizi ni za kupita, na kwa kuwa taasisi nyingi za mikopo zimefunguliwa, ukitaka kukopa milioni 200 hata 300 unapata.
Sasa baadhi wanatumia nyadhifa zao kupata mikopo na kufanya shughuli zao wakati wetu hayo hayakuwapo.
Raia Mwema: Lakini wakati wenu hapakuwa na mgogoro wa maslahi kati ya shughuli binafsi za kiongozi na dhamana unayopewa na Taifa. Hilo huoni ni tatizo kwa wakati huu?
Paul Kimiti: Zamani masharti ya uongozi yalikuwa magumu sana na hasa walipotafsiri uongozi ni mke na mume.
Masharti hayo yalifanya watu washindwe hata kufanya maendeleo kwa ajili yao. Ilikuwa ni kama wewe shughulikia kazi uliyotumwa mengine ni baadaye.
Na hiyo ilifanya watu wa-concentrate sana kwenye kazi za ofisi lakini sasa tulipoona binadamu aishi kwa mkate peke yake mpe nafasi naye afikirie maisha yake ya baadaye.
Sasa katika ruksa hiyo wengine wana-over do. Kwa kweli nasema bila kuficha wengine wana-over do kwamba wanafanya vitu ambavyo inakuwa kama kufuru. Sasa ule kwa kiasi siyo unakula hadi unasaza na kutema.
Raia Mwema: Una ushauri gani kwa viongozi walioko madarakani kuanzia wakuu wa mikoa na mawaziri, nafasi ulizowahi kutumikia kwa mafanikio.
Paul Kimiti: Nasema kazi ya kwanza ni kutumikia wananchi. Haya mengine ni matokeo. Tunajua watu wetu bado ni masikini na hivyo tutambue kuwa umasikini huo ni sehemu yetu.
Hii ni kazi ngumu lakini ni muhimu tuifanye. Ni ngumu kwa sababu mbili. Kwanza ni mazingira ya sasa na siasa zetu hizi za sasa. Mfumo wa soko huru, ambao si wa Ujamaa; tena ni mixed economy, kila mtu atabeba mzigo wake mwenyewe.
Sasa ukishafika hapo ndiyo kila mmoja anasema mzigo wangu naubeba mwenyewe na wengine wabebe mizigo yao. Kwa utaratibu huo hatufiki mahali popote; kwani kuna wengine hawana uwezo, wataanguka na mizigo yao na lazima awepo mtu wa kumsaidia ili hatimaye wote tufikishe mizigo yetu kwa pamoja.
Hiyo ndiyo kazi tuliyonayo. Ni kubwa lakini pole pole inaweza kubadilika.
Raia Mwema: Una ushauri gani kwa vyama vya siasa na wanasiasa, kikiwamo chama chako -CCM.
Paul Kimiti: Chama chetu kinaweza kuwa na matatizo ya aina mbili. Kwanza commitment ya wanachama.
Wanachama committed siku hizi si wengi. Wanachama ambao tunawapata sasa ni wa papo kwa papo tofauti na wale wa zamani ambao imani na misingi ya chama wanaifahamu na wanapikwa kwa miezi mitatu, wakiingia kwenye chama commitment yao ni ya kiwango cha juu.
Lakini mfumo wa vyama vingi umetufikisha mahali tushindane, wapinzani wasije wakawachukua wote. Ndiyo maana tunaingiza watu wengine si wanachama hasa. Wameingia ili kuchukua kadi tu.
Siku hizi nashukuru CCM wanataka kurudisha utaratibu wa kuchukua wanachama kwa kuwapa kozi-mafunzo waelewe madhumuni, misingi na shabaha ya chama.
Ili pole pole tukishajenga chama tutaweza kuzungumzia juu ya aina ya wanachama tulionao kwamba huyu ana imani kubwa. Kinyume cha hapo utaona mtu huyu anaingia hapa leo, kesho anatoka kwa kuwa hana imani.
Lakini pia hiyo inaingiza tatizo kwa viongozi, unaweza kupata kiongozi asiye na imani pia na huyo unapomtia msukosuko leo kesho anatoka anakwenda chama kingine.
Wakati mwingine watu wanasema ni mabadiliko ya dunia, mazingira yanabadilika. Lakini tuzidi kuhimiza wanachama wabadilike wawe na commitment.
Lakini la mwisho ni wivu na mashindano, sasa wivu ukishaingia kwa nini fulani yuko pale na mimi sipo pale, ndiyo ugomvi unaanzia hapo na Mwalimu Nyerere aliwahi kusema chama kinaweza kusambaratika. Chimbuko la kauli yake hiyo ni huu utaratibu wa kushindana.
Kushindana nani aingie pale na kwa misingi gani hawaangalizi uwezo lakini wanaangalia yule akiwapo pale atanisaidia nini mimi. Sasa ukifika hapo utapata matatizo makubwa sana katika utendaji.
Lakini tutaendelea kusaidiana sisi wengine tumekwishaamua kupumzika na kila mmoja ataamua kwa wakati wake na mimi nasema ndani ya Chama na bungeni, ni vizuri kuwa na mchanganyiko.
Wawepo watu wenye rika kubwa, wazee na vijana lakini pia tusilazimishe mtu kutoka. Yeye mwenyewe aone ametumikia vya kutosha atoke, lakini pia kuna hatari unaweza kutaka usitoke ukalazimishwa kutoka na hiyo si vizuri.
Raia Mwema: Umeamua kustaafu, Mwalimu alipong’atuka alikwenda kulima. Wewe umejiandaa na shughuli gani?
Paul Kimiti: Mimi kitaaluma ni bwana shamba, nina master’s degree (shahada ya uzamili) katika sayansi ya kilimo.
Nimekuwa nikijishughulisha na kilimo. Nina shamba Mkuranga la heka kama 50, kule nyumbani (Rukwa) na napenda zaidi kuwa katika field yangu mwenyewe lakini pia naweza kutoa ushauri wa kitaalamu.
Unajua unaweza kukaa na vijana ukawafunza wakawa wanafanya kazi ya consultancy na wewe ukawa kama mshauri mkuu.
Lakini pia field yangu kwa kweli tangu nikiwa mtoto ni kilimo. Nilikipenda sana tangu nikiwa shule ya msingi.
Raia Mwema: Ukiwa mtaalamu wa masuala ya kilimo, unazungumziaje uamuzi wa Serikali kuibuka na kauli mbiu ya Kilimo Kwanza?
Paul Kimiti: Naamini huu ni mwendelezo wa kauli mbiu za siasa ni kilimo, kilimo cha kufa na kupona katika ubunifu mpya. Ubunifu wenye kwenda na wakati kwa sababu kwa kiasi kikubwa sekta binafsi imeshirikishwa katika kauli mbiu hii ya sasa.
Kwa hiyo, naamini kwamba kutakuwa na matokeo bora zaidi katika utekelezaji wa kauli mbiu hiyo, lakini jambo moja la kusisitiza ni lazima watendaji husika wafahamu na waamue kwa dhati kusimamia utekelezaji wa kauli mbiu hii.
Nchini hapa si jambo jipya kuwa na operesheni mahsusi za kilimo, lakini uzoefu unaonyesha kuwa mafanikio ya kiwango cha juu hupatikana kama kunakuwa na usimamizi mzuri na pia ni muhimu kuwa na muda mahsusi wa kujipima kuhusu utekelezaji wa malengo husika.
Lazima kujipima katika kipindi hiki cha mwaka mmoja au miwili; kwa mfano tumetekeleza Kilimo Kwanza kwa kiwango gani, tumekosea wapi na tufanye nini.
Na kwa kweli matumaini yapo, tayari ipo miradi mahsusi ya kilimo cha umwagiliaji inayoshirikisha wananchi wilayani, maarufu kama DADPs (District Agricultural Development Programs). Katika hali ya kuwa na miradi kama hiyo na kauli mbiu hii ya Kilimo Kwanza, ni wazi kuwa tayari kuna mwanzo mzuri.
Kwa hiyo kinachohitajika ni mwendelezo katika usimamizi wenye ari kubwa. Naamini kuwa katika miaka ya hivi karibuni tumepata vijana wengi wataalamu wa kilimo kutoka Chuo Cha Kilimo Sokoine, Morogoro au hata kutoka vyuo vingine. Hivyo matumaini yangu ni makubwa tu katika enzi hizi za Kilimo Kwanza
