MWENYEKITI wa Umoja wa Vijana CCM Mkoa wa Arusha, James Ole Millya sasa yuko katika "mazingira magumu kisiasa" baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoani hapa kuifuta kesi iliyokuwa ikimkabili Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka, kwa maelezo kuwa mbunge huyo hakuwa na kesi ya kujibu.
Kesi hiyo ilifunguliwa mapema mwaka jana na Jamhuri baada ya Millya kulalamika kupigwa ngumi na kutishiwa kwa bastola na mbunge huyo wa Simanjiro wakati wakiwa wilayani Monduli katika mkutano ulioitishwa na Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa kuhusu masuala ya elimu kwa jamii ya wafugaji.

MWENYEKITI wa UVCCM Mkoa wa Arusha, James Ole Millya
Sendeka anadaiwa kumpiga ngumi Millya, na kisha kumtolea bastola baada ya kutokea malumbano baina yao wakati wa kipindi cha mapumziko cha mkutano huo uliokuwa ukifanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Ualimu cha Monduli, Januari 9, 2009.
Baada ya mapambano makali ya kisheria mahakamani, yaliyodumu kwa mwaka mzima kati ya upande wa mashitaka, ukioongozwa na Wakili wa Serikali, Hashim Ngole na utetezi ukiongozwa na wakili Mpaya Kamara na jopo la mawakili watano, hatimaye mahakama ilikubaliana na upande wa utetezi kuwa mbunge huyo hakuwa na kesi ya kujibu katika hukumu iliyosomwa Machi 5 mwaka huu.
Mawakili wengine waliokuwa wanamtetea Sendeka ni Ezra Mwaluko, Michael Ngalo na Modest Akida.
Hukumu hiyo ilisomwa na Hakimu Devotha Msoffe akimwakilisha hakimu aliyesikiliza kesi hiyo, James Karayemaha ambaye, hata hivyo, alihamishiwa kikazi wilayani Mpwapwa mkoani Dodoma kabla ya kuhitimisha kesi hiyo.
Katika hukumu yake, hakimu huyo alieleza kuwa mahakama haioni sababu ya Sendeka kujitetea kwa kuwa ushahidi uliowasilishwa mahakamani ulikuwa na mapungufu mengi ya kisheria; huku shahidi wa kwanza wa upande wa Jamuhuri, ambaye ni Millya mwenyewe, akitoa maelezo tofauti mahakamani kuhusu alipigwa sehemu gani ya mwili wake.
Alisema katika maelezo yake polisi, Millya alieleza kupigwa kofi la kushoto lakini wakati akitoa ushahidi wake mahakamani alieleza kuwa mshitakiwa Sendeka alimpiga ngumi upande wa kulia; huku akisahau maelezo mengine kuwa alimtishia kwa bastola.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka
“Kwa mazingira hayo, ni vigumu kwa mahakama kufahamu mlalamikaji alipigwa sehemu gani ya mwili wake; hivyo ushahidi wake unakosa nguvu ya kisheria”, alisema.
Hata hivyo, muda mfupi baada ya kusomwa kwa hukumu hiyo, wazee wa kimila (Lagwanani) kutoka jamii ya Kimasai ambao walikuwepo mahakamani kufuatilia kesi hiyo, walizungumza na waandishi na kutoa maoni yao; huku wakimtuhumu Millya kwa kuvunja miiko ya asili ya jamii hiyo kwa kuamua kupeleka malalamiko yake mahakamani badala ya kusuluhishwa kimila.
Kiongozi wa kwanza wa kimila kuzungumzia suala hilo alikuwa Yohana ole Tiamongoi ambaye pia ni katibu wa baraza la wazee hao wa kimila wa Kimasai mkoani Arusha. Tiamongoi alieleza wazi kuwa hawakufurahishwa na hatua ya Millya kukataa kusuluhishwa kimila baada ya kutofautiana na Sendeka.
Alisema jamii ya Kimasai imejiwekea utaratibu wa kumaliza tofauti zinazojitokeza katika makundi mbalimbali ya kijamii kama vijana, watu wa rika la kati, wanawake na wazee, na utaratibu huo umekuwa ukitumika kwa karne nyingi; hivyo Wamasai kujenga jamii ambayo imeweza kudumumisha mila na desturi zake hadi leo.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo wa kimila, wakati mgogoro huo ulipotokea, wazee wa kimila kutoka wilaya za Monduli, Simanjiro, Ngorongoro na Longido, viongozi wa dini (maaskofu Thomas Laizer na Askofu Mameo wa Dayosisi ya Morogoro ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania - KKKT) walijaribu kuwasuluhisha nje ya mahakama lakini Millya aligoma.
Alisema Millya hakupaswa kupeleka shauri hilo katika vyombo vya sheria; hasa katika kipindi hiki ambacho Mwenyekiti huyo wa Umoja wa Vijana ametangaza nia ya kugombea ubunge katika jimbo la Simanjiro katika uchaguzi wa mwaka huu.
“Kama kiongozi wa vijana, alipaswa kuonyesha mfano kwa vitendo kwa kusikiliza ushauri wa wazee na kumaliza shauri hilo nje ya mahakama……sasa kama hawezi kusamehe wenzake atakuwa kiongozi wa aina gani?”, alihoji mzee huyo wa kimila.
Tiamongoi aliongeza: “Hata viongozi wa vijana wa rika lake la Korianga walijitahidi sana kuzungumza naye ili suala hilo limalizwe kimila, lakini bado aligoma na hiyo inaonyesha wazi kuwa kijana huyo amepuuza mila na desturi zetu za watu kuheshimiana”, alisema.
Kiongozi mwingine aliyezungumzia suala hilo ni Joel Lesongoyo aliyesema kuwa jamii ya Wamasai imejijengea utamaduni wa watu kupendana, kuheshimiana na kushikamana na linapotokea tatizo lolote huchukuliwa kama changamoto kwa jamii na watu wote kwa rika zao hushirikiana kumaliza tatizo hilo.
“Kwangu mimi itakuwa vigumu sana kwa Millya kuwashawishi watu wa Simanjiro kuwa yeye ni moja wetu na anataka kuwa kiongozi wa umma wakati ameshindwa kutoa ushirikiano wa kumaliza tatizo dogo kama lililotokea”, alisema.
Lesongoyo alisema kimsingi suala hilo litamgharimu Millya katika harakati zake za kuwani ubunge wa jimbo la Simanjiro na kuongeza kuwa watu wengi hawakufurahishwa na uamuzi wake wa kumpeleka Sendeka mahakamani.
“Siwezi kulisemea suala hili kuwa kuna shinikizo la kisiasa kutoka kwa makundi hasimu, lakini ukweli unabaki kuwa ni Millya binafsi ndiye aliyekuwa na maamuzi ya mwisho kuhusu mgogoro baina yake na Mbunge Sendeka”, alisema.
Hata hivyo, akizungumza na Raia Mwema kwa njia ya simu, Millya alipuuza madai yanayotolewa kuwa kesi hiyo itamgharimu kisiasa na kueleza kuwa alifikia uamuzi wa yeye kugombea ubunge kabla hata ya kutokea ugomvi baina yake na Sendeka.
“Madai hayo hayana msingi wowote na nia yangu ya kuwania ubunge wa jimbo la Simanjiro kwa tiketi ya CCM ni ya muda mrefu kabla hata ya kesi iliyotokea. Kwa hiyo nia yangu iko palepale, na wala hukumu ya kesi hii haiwezi kunizuia katika malengo yangu ya kisiasa”, alisema.
Mwenyekiti huyo wa jumuiya ya UV-CCM aliongeza kuwa hata wazee wanaozungumza kuwa nitakuwa nimejiweka katika mazingira magumu kisiasa ni wale ambao wanamuunga mkono mbunge wa sasa (Sendeka) na wote hao walikuwa wanahudhuria mahakamani kufuatilia kesi hiyo si kama wazee wa kimila bali marafiki wa mbunge huyo.
Alisema mpaka kufikia uamuzi na kutangaza nia ya kugombea ubunge, alifanya utafiti wa kutosha kuwa anakubalika miongoni mwa rika tofauti kwa wananchi wa jimbo la Simanjiro ambao kimsingi ndiyo wenye uamuzi wa mwisho kuhusu nani awe mbunge wao mwaka 2010.
“Tuwape wananchi wa jimbo la Simanjiro nafasi ya kumchagua mtu wanayeona anafaa kuwa mwakilishi wao….wananchi ndiyo mahakimu wazuri kidemokrasia badala wapambe kulumbana katika masuala yasiyo na msingi”, alisema Millya.
Kwa upande wake, akizungumza muda mfupi baada ya kuachiwa huru na mahakama, Sendeka aliwaeleza waandishi wa habari kuwa anashukuru mahakama imetoa maamuzi ya haki katika kesi hiyo hiyo lakini binafsi alikuwa tayari kupokea maamuzi yoyote.
“Binafsi nilikuwa radhi kupokea maamuzi yoyote yatakayotolewa na mahakama kama nilivyowaambia wenzangu tangu Januari mwaka jana kuwa waendelee na kazi zao kama kawaida kwa kuwa mahakama zetu zina hadhi ya kuaminiwa”, alisema Sendeka.
Sendeka aliongeza: “Binafsi kama Mkiristo nimewasamehe kwa nia moja wale wote waliohusika katika kutaka kunichafulia jina langu na hadhi yangu miongoni mwa wanajamii, lakini napenda kuweka wazi kuwa nitashauriana na wenzangu tuone jinsi waliohusika watakavyosafisha jina langu”, alisema.
Mbunge huyo jana Jumanne alitarajiwa kupokelewa kishujaa katika mji wa Orkesmet ambako ni makao makuu ya wilaya hiyo katika mkutano mkubwa wa hadhara ulioandaliwa na wafuasi wake.
