WIKI hii naamua kufungua sura mpya katika safu hii nikiwa na nia madhubuti ya kujadili kwa undani masuala yanayohusiana na shughuli kuu ya kisiasa kwa mwaka huu: Uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Hii ndiyo itakuwa shughuli kuu kwa muda wote uliosalia hadi mwisho wa mwaka huu wakati Watanzania watakapopiga kura kuwachagua wenzao watakaowaongoza kwa muhula wa miaka mitano kama ilivyopangwa na Katiba ya nchi, na kisha wakuu waliochaguliwa watakapokuwa wakiunda serikali mpya.
Kwa hakika, hiki kitakuwa kipindi muhimu katika maisha ya Taifa letu, kwa sababu uchaguzi huu unabeba maana nzito katika kujenga utawala wa kidemokrasia ili kuhakikisha kwamba nchi yetu inatawaliwa kwa haki na kwamba waliomo madarakani wameingia humo kwa ridhaa ya wananchi na watafanya kazi zao kwa kuweka maslahi ya wananchi mbele ya kitu cho chote kingine.
Lakini yote hayo ni nadharia; ndivyo ambavyo mambo yangepaswa yawe kwani ndivyo misahafu yote inavyosema, na ndivyo watawala wetu wanavyodai kila siku. Ni wazi kwamba hakuna mtawala ye yote, hata angekuwa mbovu wa gredi ya mwisho, atakayethubutu kusema lo lote lililo kinyume cha hayo niliyoyasema hapo juu.
Ukweli ni kitu kingine kabisa. Katika kipindi hiki tutashuhudia pilika nyingi, shughuli kem kem na hekaheka za kila aina. Wanasiasa wa kila sampuli na wapambe wao watapita huku na huko kujinadi, kubembeleza, kuhonga, kulaghai, kuahidi, kutishia, na kila aina ya hila alimradi tu wao au wanaowataka wachaguliwe wanachaguliwa.
Katika hekaheka hizi tutashuhudia ukweli kwamba matendo ya wanasiasa hao yatakuwa ni matendo ya kuvunja nguvu ya demokrasia, ingawa wanasiasa hao na wapambe wao watakuwa wanadai kwamba wanachofanya ni kuimarisha demokrasia.
Ni muhimu, kwa hiyo, kwa wapenda demokrasia wote kuwa macho na kuwachunguza wanasiasa na wapambe wao na kubaini matendo yote yanayoweza kutuelekeza katika kubatilisha misingi ya demokrasia badala ya kuiimarisha.
Umuhimu wa kuwa macho kuhusu mambo yote yanayohusu uchaguzi unatokana na utakatifu wa dhana ya uchaguzi, utakatifu ambao hatuna budi kuutambua na kuuheshimu kwa sababu tunauelewa utakatifu huo.
Utakatifu wa uchaguzi unatokana na kukubali kwetu (kama kweli tumekubali) kwamba tunalazimika kuweka serikali itakayotutawala sisi, nchi yetu na mali zake, na kwamba serikali hiyo haina budi itokane na ridhaa yetu, ridhaa itakayodhihirishwa kupitia kura zetu.
Dhana ya utakatifu wa uchaguzi inavurugika vibaya pale uchaguzi unapokuwa si uchaguzi tena bali sakata la vurugu, ubazazi, ulaghai na udanganyifu. Utakatifu wa uchaguzi unaingia najisi pale washindani na wasaidizi wao wanapoacha misingi ya ushindani wa kiungwana na kuingia katika vurumai zisizo na kichwa wala mkia.
Tukae tukijua, na tuendelee kukumbushana, kwamba uchaguzi ukiisha kutiwa najisi, jamii inakuwa haina imani nao tena, na kupoteza imani katika utakatifu wa uchaguzi ndicho chanzo cha kutafuta mfumo mbadala wa kupata uongozi, na mara nyingi mfumo huo mbadala ni ule unaotegemea machafuko na mauaji, ambamo mwenye mabavu ndiye anachukua anachokitaka.
Kuvuruga uchaguzi kwa niia yo yote ile ni dhambi kubwa na ambayo ingestahili kukomeshwa kwa adhabu sawa na ile wanayostahili wahaini. Tumeshuhudia jinsi ambavyo uvuragaji wa uchaguzi unavyoweza kusababisha mauaji ya mamia ya watu na uharibifu wa mali na uchomaji moto wa miji na vijiji.
Sasa, hebu tujisaili kidogo kuhusu mantiki ya mambo haya: Kama wahaini wanaotaka kuiondoa serikali madarakani kinyume cha utaratibu halali wanahukumiwa kunyongwa, ni kwa nini adhabu hiyo hiyo isitolewe kwa wale wanaoiba uchaguzi huku wakijua kwamba matendo yao yanaweza kuwa chanzo cha vifo vya mamia ya raia wenzao?
Kujaribu kuiondoa serikali iliyopo madarakani kwa nguvu za kijeshi (coup d’etat), kwa mfano, ni aina ya uhaini na katika nchi nyingi adhabu yake ni kifo. Kuvuruga uchaguzi, kuiba kura, kubadilisha matokeo, kukana utashi wa wapiga kura na kuwanyima uhuru wa kuchagua kwa kuwachagulia wasichokitaka… ni uhaini ambao katika mazingira mengi unaweza kuangamiza taifa zima au kusababisha maafa yasiyo kifani. Kama tunakubali adhabu ya kifo kwa ajili ya makosa fulani, ni kwa nini kosa hili nalo lisihusishwe na adhabu hiyo?
Tukizichunguza nchi nyingi za Kiafrika ambazo zimewahi kupatwa na machafuko na vita za ndani, mara nyingi tutagundua kwamba miongoni mwa vyanzo vikuu vya machafuko hayo ni uchaguzi ulioingia najisi. Mantiki yake ni rahisi kuielewa: Kama tumekubaliana kwamba uchaguzi ndiyo njia pekee mwafaka ya kupata uongozi wetu, halafu wewe unahakikisha kwamba hata wananchi wangemtaka Musa, watapewa Juma na watalazimishwa wamkubali Juma, ukweli ni kwamba wewe unataka vita.
Bila shaka najisi ndani ya uchaguzi huambatana na aina nyingine nyingi za uozo, zikiwamo kile kinachoitwa ufisadi. Jamii yenye wanasiasa na wapambe wanaopotosha matokeo ya kura, au wanaofanya kwa njia moja au nyingine uchaguzi upoteze maana yake, vile vile inakuwa ni jamii iliyojaa rushwa, ulaghai, ubabe, uonevu na ubabaishaji.
Waama lingekuwa jambo jema endapo wizi wa uchaguzi ungetokana na ari kubwa ya kuwatumikia wananchi kiasi kwamba mwanasiasa anayewapenda wananchi wake atafanya kila jitihada, pamoja na wizi, ili tu apate fursa ya kuwatumia watu wake. Lakini huo ni wendawazimu, kwani hakuna kitu kama hicho.
Wizi wa kura husababishwa na wizi mkubwa zaidi, wizi wa mamlaka juu ya nchi, watu wake na rasilimali zake, uwezo wa kuamuru nchi nzima, watu wake na rasilimali zake, na kuzifanyia hizo rasilimali unachotaka wewe na kundi dogo linalokuzunguka bila kuulizwa na mtu ye yote. Huo ndio wizi unaosababisha wizi wa uchaguzi.
Rika langu tulipokuwa kijana tungeambiwa kwamba mkuu wa nchi yetu alikuwa ni mwizi ambaye anatuibia kwa kuchukua rasilimali za Tanzania na kuzifanya zake yeye na familia yake, tungekataa kwani dhana hiyo ilikuwa haiingii akilini. Lakini sasa tunajua kwamba mkuu wa nchi anaweza kuwa mwizi wa rasilimali, na kwa maana niliyoitoa hapo juu mtu kama huyo lazima ataiba uchaguzi.
Kama nilivyosema mapema, nchi nyingi zilizokumbwa na machafuko ni zile zilizotawaliwa na wanasiasa wezi wa aina zote, wezi wa rasilimali za nchi zao, na kwa sababu hiyo wezi wa uchaguzi. Ni hao hao wanasiasa ambao wanakuwa ndio chanzo cha ghasia.
Kama ye yote anashuku ninachokisema hapa, ajikumbushe kidogo mfano wa jirani zetu wa Kenya, kama amekwisha kusahau yaliyotokea visiwani Zanzibar miaka michache iliyopita, lakini anaweza pia kuzitazama nchi nyingine nyingi za Afrika zilizopata misukosuko ya kila aina: Sierra Leone, Liberia, Chad, Kongo-Kinshasa, Kongo-Brazzaville, Chad, CAR, Niger, Algeria, na kadhalika.
Ndiyo maana nashindwa kuafikiana na baadhi ya serikali za Afrika, ikiwamo Serikali ya Tanzania, wanaolaani mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika nchini Niger kwa kumwondoa rais wao, Mamadou Tandja. Huyu rais alikwisha kufanya coup d’etat yake kwa kulazimisha mabadiliko ya katiba ili aendelee kutawala.
Kwa watu wengi waliofuatilia sakata la Niger, Afrika inapswa kuwapongeza wanajeshi wa Niger kwa kuinusuru nchi yao na utawala wa dikteta Tandja. Watawala wa “kiraia” wanapojifanya makamanda na kutaka kutawala kwa amri, huo unakuwa ni mwaliko kwa ujeshi kuchukua madaka; kwani hakuna anayeweza kuamuru kuliko kamanda.
Inapotokea kwamba katiba inachezewa jinsi anavyotaka mtawala, akaibadilisha anavyotaka na kujifanya mtawala wa maisha, inawezekana nchi ikakosa asasi yo yote inayoweza kukabiliana na hali hiyo isipokuwa jeshi peke yake. Katika hali kama hiyo, jeshi linakuwa na wajibu wa kizalendo wa kulinusuru Taifa.
Kma kweli hatutaki vyombo visivyokuwa vya kiraia na kidemokrasia kuingilia utawala wa nchi zetu, hatuna budi kuhakikisha kwamba vyombo vya kiraia na kidemokrasia vinatimiza majukumu yake inavyopasa, na mojawapo ya vyombo hivyo ni hiki chombo kitakatifu, uchaguzi.
Katika safu hii nitakuwa najadili masula mbali mbali yahusuyo mchakato mzima wa uchaguzi wa mwaka huu, kila mara nikiwa najaribu kukumbusha na kutanabahisha kuhusu madhara tunayoweza kukumbana nayo iwapo tutawaruhusu watu wenye nia mbaya kunajisi mchakato wa uchaguzi.
Itaendelea
