WAKATI nikilalamikia misimamo inayoiumiza demokrasia nchini mwetu, mambo yamekuwa yakienda kwa kasi kubwa sana kuelekea uchaguzi wa Oktoba. Wanasiasa (wa kweli na bandia) wanapitapita kila mahali wakijinadi, wakibembeleza, wakidanganya, wakijipendekeza, wakifitiana, wakiloga, wakijidhalilisha, alimradi wakifanya kila wawezalo ili wajihakikishie kura.
Ingawa imebaki miezi mitatu mizima kabla ya siku ya kupiga kura, kiwewe kimeingia miongoni mwa wagombea watarajiwa, na pilika zilizoshuhudiwa hadi sasa zimewafanya hata watu ambao hawana mazoea ya kusaili mienendo hiyo kuanza kujiuliza ‘kulikoni?’ Utadhani ghafla umeingia ugonjwa wa ajabu unaowafanya watu ambao kwa kawaida wana akili zao timamu wazitelekeze akili zao na waingie mtaani wakiwa uchi, kufanya madudu yasiyokuwa na staha wala haya.
Tumepata taarifa za wanasiasa na wapambe wao kukamatwa wakidaiwa kutoa rushwa kinyume cha maangalizo waliyopewa na viongozi wao na maonyo yaliyotolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU). Picha inayopatikana hivi sasa ni ya watu walionyweshwa mvinyo mkali ambao athari yake kwa mnywaji ni kwamba hasikii tena analoambiwa na mama wala baba; atadharau maonyo ya mkuu ye yote yule iwapo atayaona kama yanayolenga kumnyima raha anayoihisi katika wendawazimu alimotumbukia.
Leo tunashuhudia wakuu wa ngazi mbali mbali, wakiwamo maofisa wa serikali wenye dhamana ya kulinda amani, wakiwa msitari wa mbele katika usambazaji wa fedha haramu na vifaa vingine vya hongo, kana kwamba hawajasikia mbiu iliyopigwa, au hata kama wamesikia wanajua hizo ni porojo tu na hakuna anayeweza kuwakemea, kwa sababu wote wameingia katika mkumbo huo.
Tumeshuhudia maofisa wa chama-tawala wakikihujumu chama chao wenyewe kwa kuchapisha na kusambaza kadi bandia za chama hicho, bila shaka kwa kutaka kuzitumia kuwapa ushindi wagombea wanaowapendelea. Hili linafanyika huku wakuu wa ngazi za juu katika chama hicho wakionyesha kutokujali sana kwamba chama chao kinahujumiwa kwa njia hii. Nahisi mtazamo wao ni kwamba hakuna kilichoharibika alimradi watapa kura za kuwaweka pale wanapotaka kuwa.
Kwamba haya yote, au angalau yaliyo mengi na makubwa, yanafanyika ndani ya chama-tawala, ni kielelezo cha jinsi nchi yetu inavyoendeshwa. Chama hiki ndicho kinachozaa serikali ya kututawala sisi, na familia zetu na mali zetu, na kutuandalia mustakabali wa watoto wetu, na watoto wao, na watoto wa hao pia.
Kama hivi ndivyo unavyofanyika uchaguzi ndani ya chama hicho tuambizane ukweli, kuna tumaini gani kwamba chama hicho kinaweza kuweka serikali madarakani na ikaweza kuwatumikia wananchi wa Tanzania?
Nauliza swali hili nikijua kwamba ni swali linaloitwa swali la ‘retoriki’ kwa maana kwamba linajitosheleza na wala halihitaji jibu. Lakini ninaliuliza kwa nia ya kuwafanya wakuu wa chama hicho wazinduke katika ndoto zao, na wajue kwamba wanakotupeleka siko.
Ni bora, basi, tungeambizana kwamba kwa kuwa mambo yamekuwa mazito na utamaduni wa kununua wapiga kura tumekuwa nao kiasi kwamba sasa hatuwezi kuuondoa, ni vyema kuendelea hivi hivi kama tulivyo, halafu huko mbele ya safari tutapata fursa mwafaka ya kuketi na kulijadili suala hili kwa nia ya kulitafutia dawa.
Hali hii ya kutangaza juhudi za TAKUKURU kuwakamata watu wanaoshukiwa kutoa rushwa, mimi naamini halina maana kubwa. Ni mchezo wa kuigiza kwa sababu uoza ulioenea katika chama hicho hauwezi kukomeshwa kwa kutumia asasi ya dola.
Ulevi wa baadhi yetu umefikia viwango vya kutisha. Hata hivyo, hatuna budi kukubali kwamba tumeuendekeza sisi wenyewe, na tumeulea na tukauvumilia huku tukiuona ukikua mwaka hadi mwaka, muongo hado muongo, hadi leo tu walevi ‘chakari’.
Laiti ingekuwa rahisi kuwalaumu walevi hawa wa leo, ningefanya hivyo kwa furaha kuu, na ningejua majina ya kuwabandika ya kufanana na ulevi wao huo. Tatizo hapa ni kwamba walevi tunaowashuhudia leo wakihaha mitaani na vijijini ni walevi wa kurithi, ambao wamerithishwa ulevi huo kutoka kwa wale waliowatangulia na michakato waliyopitia huko walikotoka.
Uongozi uliopita ulishindwa kukemea vitendo hivi kwa sababu vilionekana kama vinawasaidia viongozi wa wakati huo kuingia au kubaki madarakani. Hebu tujiulize: Tangu tuingie upya katika siasa za ushindani wa vyama ni shilingi bilioni ngapi za rushwa ziliingizwa katika kampeni za uchaguzi, na kiasi gani katika hizo zilitokana na biashara haramu, kama vile mihadarati?
Je, wanasiasa waliochaguliwa kwa fedha za mihadarati wanaweza wakawa ndio walezi wa vijana wetu na wakawalinda dhidi ya biashara hiii ya kifo?
Hili ni swali moja tu, na linalohusu eneo moja tu, lakini maswali mengine mengi yangeweza kuulizwa katika maeneo mengi, na majibu yake yangeonyesha jinsi ambavyo wanasiasa wetu wanavyotupeleka hovyo.
Leo tunapokea taarifa za vituko vya ajabu: watu kugawa fedha kama njugu; wanasiasa kukamatwa na TAKUKURU wakishukiwa kugawa rushwa, na wanasiasa kuwakamata TAKUKURU kwa kuwadhania ni majambazi; waandishi wa habari kuitiwa polisi wakiambiwa ni majambazi, waandishi wa habari kujifanya wenyewe ni maofisa usalama au maofisa wa TAKUKURU, na kadhalika.
Hizi zote, na nyingi nyingine ambazo tumezipata, ni dalili ya uoza mkubwa mno ambao unaendelea kusambaza uvundo katika mifumo yetu ya siasa wakati watawala wetu wanaonekana kama wasiokuwa na fununu ni nini wafanye kuzuia hali hiii isiendelee kutanda.
Tumefika mahali pabaya, na iwapo hatua madhubuti hazitachukuliwa, basi tushauriane ili tuanze kufanya maandalizi ili siku jahazi litakapogonga mwamba na kuanza kutota, tujue nini la kufanya.
Kwa mwenendo huu, hakika tunaelekea mwambani, na asiyeliona hilo ama ni kipofu kinara wa vipofu, ama ni miongoni mwa wale wanaotupeleka huko huko mwambani.
Hebu tuangalie ushahidi. Tulio wengi tumekubaliana kwamba utoaji na upokeaji rushwa katu haviendani na demokrasia, haki wala amani katika jamii. Sababu zake zinajulikana: Haiwezekani kuwa na viongozi waliopatikana kwa uuzaji na ununuzi wa kura, halafu viongozi hao wakafanya kazi ya kuwasaidia wananchi kuondokana na umasikini. Hii inakuwa ni biashara, na haihusiani kabisa na maslahi ya wananchi.
Miaka mingi iliyopita niliwahi kujaribu kuonyesha kwa mifano inayofikirika ni jinsi gani tajiri mmoja, au kikundi kidogo cha matajiri, wa hapa nchini au wa nje ya nchi, anaweza/wanaweza kuamua kushiriki katika soko la kura tulilolianzisha nchini, na wakashinda kwa sababu tumeruhusu uchaguzi wetu uwe ni gulio ambalo ndani yake kila mwenye uwezo wa kifedha anaweza kushiriki. Hali hii, si tu kwamba imeendelea kushamiri nchini, bali imekuwa mbaya zaidi.
Tunayo bahati ya muda kutokana na ukweli kwamba mwaka huu chama-tawala kinafanya kazi ya kuvurugana katika ngazi za chini, za udiwani na ubunge. Nafasi ya juu kabisa, ya urais, haishindaniwi ndani ya chama hicho. Hali hii inatoa nafuu kwa maana ya kupunguza ngazi za malumbano na kila aina ya hila tunazozishuhudia katika ngazi za udiwani na ubunge.
Lakini mwaka 2015 hali itakuwa ntofauti kabisa, kwani wako watu wengi ndani ya chama hicho chenye fujo wanaosemekana kwamba wamejipanga kuwania kuteuliwa kugombea urais. Kama haya tunayoyashuhudia leo ni ishara za awali za yale yatakayotokea miaka mitano kutoka leo, basi, wanaoamini kwamba sala husaidia waanze kusali, kwani kutawaka moto. Watavurugana, kisha watatuvuruga na sisi.
Ningependa kukumbusha tena kwamba haya yote yanatokana na kuwa na vyama visivyokuwa na itikadi wala falsafa, na hasa chama-tawala ambacho kimetupilia mbali itikadi, falsafa na sera na sasa kimebaki ni chombo cha watu kugawana vyeo na ulaji.
Pasipokuwa na falsafa wala itikadi ni vigumu kukubaliana nani atangulie mbele na wengine wamfuate, kwani zinakuwa ni mbio za ulaji ambamo tija hutokana na kuwahi.
TAKUKURU na waendelee kuwashika hao wanaowashika. Ningependa wanishangaze, lakini hawawezi kwani nayaelewa mazingira wanamofanyia kazi zao: Hawaiwezi kazi hii kwa sababu wanafanya kazi isiyokuwa yao.
Hii ni kazi ya siasa iliyotelekezwa na wanasiasa waliolewa mvinyo huu ambao athari zake tunazishuhudia hivi sasa.
Itaendeleap
