DUNIA inatajwa kuwa na maajabu saba! Moja ya maajabu hayo ni Kreta ya Ngorongoro ambayo imekuwa moja ya vivutio vya utalii si tu katika eneo la Afrika Mashariki bali duniani na hivyo kuiweka Tanzania katika ramani ya ulimwengu. Hifadhi hiyo imeletea sifa si haba kwa Tanzania katika sekta ya utalii na kila mwaka mamia ya wageni kutoka mataifa mbalimbali ya nje wamekuwa wakimiminika kuja Tanzania kujionea maajabu yake.
Lakini wakati dunia ikiamini kuwa Ngorongoro ni ajabu la saba la dunia hali ni tofauti kwa wananchi wa Wilaya jirani ya Karatu ambao wanaamini kuwa maajabu ya nane ya dunia yatatokea mwaka huu lakini katika uwanja wa siasa nchini kwa mgombea wa nafasi ya Urais kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Dk. Wilbroad Peter Slaa kushinda kiti hicho katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu. Dk.Slaa ambaye pia ni Katibu Mkuu wa CHADEMA aliteuliwa na kamati kuu ya chama chake iliyokutana wiki iliyopita jijini Dar es Salaam kuwa mgombea wa nafasi hiyo ya Urais kupitia chama hicho.
Tangu CHADEMA kilipomtangaza kuwa mgombea Urais, Dk.Slaa amekuwa gumzo kubwa miongoni mwa wananchi na huenda kwa mara ya kwanza akatoa upinzani mkubwa kwa mgombea Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Jakaya Kikwete, tofauti na chaguzi zilizopita za vyama vingi. Imani kali ya wananchi hao wa Karatu mgombea huyo atafanya “maajabu ya nane ya dunia” inathibitishwa na zaidi na mapokezi ya kihistoria aliyoyapata Dk.Slaa Jumatatu ya wiki hii wakati aliporudi jimboni kwake na akapokewa na maelfu ya wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo.
Lakini imani ya wananchi hao pia inajengwa na uadilifu usiotia shaka wa Dk.Slaa, kushiriki katika kufichua maovu na ufisadi mbalimbali uliofanywa na watendaji wa Serikali ndani ya Bunge na kuwatumikia wananchi wa Karatu kwa miaka 15 huku akifanya mambo mengi. Dk.Slaa aliwasili Karatu Jumatatu ya Jula 26 akiambatana na viongozi wa ngazi za juu wa CHADEMA na pamoja na kuhutubia wananchi katika mkutano wa hadhara pia alichukua rasmi fomu ya chama chake ya kuomba nafasi ya kuwania uongozi wa juu wa nchi.
Siku mbili kabla ya kuwasili kwa Dk.Slaa mji wa Karatu ulikuwa katika harakati kubwa za maandalizi ya kumpokea shujaa huyo ambaye amekuwa Mbunge wa jimbo hilo kwa miaka 15 tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi hivyo kuweka rekodi ya kipekee nchini ya kuwa mbunge wa Upinzani aliyetumikia jimbo lake kwa muda mrefu. Wananchi wa mji wa Karatu na vitongoji vyake walionekana wakiwa katika vikundi vidogovidogo katika maeneo mbalimbali yakiwamo ya burudani wakijadili kuhusu hatua ya mgombea huyo kukubali kuwania nafasi ya Urais.
Katika mijadala hiyo ambayo Raia Mwema ilifanikiwa kuisikiliza kwa kuzungumza na baadhi ya wananchi, inaeleza hisia zao kuhusu uamuzi wa Mbunge wao kukubali kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba 31 mwaka huu. Moja wananchi hao ni John Zephania Lulu (56) mkazi wa kijiji cha Gekrum-Arusha kilichopo nje kidogo tu ya mji wa Karatu anaeleleza kuwa Dk.Slaa ataushangaza ulimwengu kwa kuibuka mshindi katika uchaguzi wa mwaka huu na hivyo kuvunja mwiko wa chama tawala CCM kushinda katika chaguzi zote tangu kuanzishwa tena kwa mfumo wa vyama vingi.
Lulu ambaye anajitambulisha kuwa ni mkulima na mfanyabiashara ndogondogo anaeleza kuwa mgombea huyo wa CHADEMA ni mtu mwadilifu na ambaye pia amejiwekea rekodi ya utumishi uliotukuka wakati akiwa Mbunge wa Karatu kwa miaka 15. “Wananchi wengi watampigia kura kutokana rekodi zake za utendaji kazi zinazojieleza zenyewe… pamoja na nguvu kubwa ya CCM watu watarajie maajabu ya nane ya dunia….tutaushangaza ulimwengu kwa Dk.Slaa kuwa Rais wa kwanza kutoka Upinzani miaka 50 tangu uhuru wa nchi yetu,” anasema Lulu.
Lulu anajipa matumaini kuwa hata Marekani katika uchaguzi wao uliofanyika mwaka juzi waliushangaza ulimwengu pale walipomchagua Mmarekani Mweusi wa kwanza kuwa Rais wa nchi hiyo (Rais Barack Obama) baada ya miaka 200 kupita na hivyo kuweka historia mpya. Anasema Lulu: “Katika siasa maajabu kama hayo ni ya kawaida…hakuna aliyetarajia kuwa siku moja nchi kubwa kama Marekani itaoongozwa na Rais Mweusi, lakini tayari hiyo imetokea. Sasa kwa nini Tanzania yasitokee maajabu kama hayo wakati kuna mgombea mwenye sifa kama huyo amejitokeza?”
Kuhusu utawala wa CCM, Lulu anasema huku akiungwa mkono na kundi la wenzake ya kuwa ni utawala uliojisahau kupita kiasi na hauwezi kuleta mabadiliko ambayo wananchi wanayahitaji. “CCM wameshindwa kuwatekelezea wananchi mambo muhimu, kwa hiyo tunahitaji chama mbadala kitakachounda serikali itakayosimamia masuala muhimu yanayogusa wananchi,” anasema.
Akitoa mfano, Lulu anasema mpango wa Serikali kugawa pembejeo za kilimo kwa wakulima (vocha) haukuweza kuwasadia kutokana na usimamizi mbovu wa watendaji na kushamiri kwa mfumo wa rushwa hivyo kusababisha wakulima wengi kutokufaidika na mpango huo. “Wakulima wengi hawakufaidika kutokana na mipango isiyo makini ya watendaji wa Serikali. Kwa mfano, kuletewa mbegu ambayo mkulima hahitaji au kuletewa mbegu wakati muda wa kupanda zao husika ukiwa umekwishakupita,” alisema.
Mkazi mwingine wa Karatu, Joseph Hiiti, anasema ombi lake ni kwamba Mungu ampe uhai kwanza ili aweze kushuhudia Dk.Slaa akirudisha fomu lakini pia ampe uhai ili aweze kushuhudia siku akiapishwa mara baada ya kushinda uchaguzi. “Naomba Mungu anipe uhai ili niweze kushuhudia mambo hayo ya muhimu sana kwa mustakabali wa Taifa letu. Kwanza nishuhudie Dk. Slaa akirudisha fomu yake ya kuwania nafasi ya Urais lakini pia nishuhudie akiapishwa kuwa Rias wa nchi hii,” anasema.
Kwa hakika matamanio ya wananchi hao yalitulizwa na mapokezi makubwa aliyoyapata Dk.Slaa ambayo yanaelezwa kuwa yalikuwa ya kihistoria katika Wilaya Karatu kutokana na kukusanya idadi kubwa ya watu wa kada na rika mbalimbali.
Mapokezi hayo yalianzia katika eneo la Kigogoni wilayani Monduli umbali wa kilomita 60 kutoka mjini Karatu na yalihusisha magari zaidi ya 100, pikipiki baiskeli na yalipofika kilomita tano kutoka mjini Karatu tayari maelfu ya wananchi walikuwa wamejitokeza kumpokea Dk.Slaa na viongozi wenzake hadi Uwanja wa Bwawani ulioko nje pembezoni mwa mji huo.
Msafara huo ulipowasili eneo Karatu mjini, hali ilibadilika kutokana na mamia ya watu kujitokeza na kuungana na msafara huo, hali iliyosababisha shughuli mbalimbali pamoja na biashara hasa katika Soko Kuu na zile za katikati ya mji kusimama kwa muda. Viongozi walioandamana na Dk. Slaa ni pampja na Mwenyekiti Freeman Mbowe, wabunge wa chama hicho Lucy Owenya, Grace Kiwelu, Halima Mdee na Wakurugenzi John Mrema na Wilfred Lwakatare. Katika uwanja huo idaidi kubwa ya wananchi ilikuwa imejitokeza kuwasikiliza viongozi hao huku Dk. Slaa akitumia nafasi hiyo kurudisha fomu ya kuomba ubunge akikabidhiwa ya Urais.
Akifungua mkutano huo wa hadhara Mwenyekiti Mbowe alisema kuwa Tanzania inakabiliwa na msiba mkubwa unaotokana na umasikini,ujinga na hofu inayotokana na utawala mbovu wa CCM. Alisema Mbowe: “Watanzania wenzangu, napenda kuwaeleza kuwa Taifa linakabiliwa na msiba unaotokana na maadui watatu ambao ni ujinga, umaskini na hofu kuu. Miaka 50 ya utawala wa CCM bado wananchi wetu wamepigika, hivyo tunahitaji kukombolewa.”
Alisema chama chake kimepania kwa dhati kuleta mabadiliko ya kweli ili kuwakomboa Watanzania na ndiyo maana kamati kuu iliamua kumpitisha Dk.Slaa kugombea nafasi ya Urais kwa lengo la kuing’oa CCM madarakani. “ Ni lazima nikiri kuwa maamuzi ya kumchagua kuwa mgombea wetu yalikuwa magumu, lakini kabla kufikia uamuzi huo tulifanya utafiti wa kutosha katika ngazi tofauti hadi tulipojiridhisha kuwa Dk.Slaa ana sifa za kutosha na zinazostahili kuwania nafasi hiyo,” alisema Mbowe.
Alisema baada ya kumtangaza Dk.Slaa kuwa mgombea Urais tayari mahasimu wao wakubwa, CCM, wameaanza kuwa na hofu na kuanza propaganda za kisiasa kuhusu mgombea wao. “Sasa kilichopo mbele yetu ni kuhakikisha kuwa tunapigana usiku na mchana kumnadi kwa wananchi ili aweze kushinda nafasi aliyoomba na hatimaye chama chetu kiweze kuunda serikali,” alisema. Akizungumza mara ya kwanza tangu atangazwe kugombea nafasi ya Urais, Dk.Slaa alieleza ya kuwa kabla ya kukubali kuwania nafasi hiyo alipokea ujumbe kutoka kwa watu wa kada tofauti, viongozi na wazee wa chama chake kuwa agombee nafasi hiyo. “Kama Baba wa Taifa letu Mwalimu (Julius) Nyerere alivyotuambia kuwa Ikulu si mahali pa kukimbilia, nami nilisita kidogo, lakini baada ya kutafakari kwa kina nilikubali maombi yao kwa kuwa sauti ya watu ni sauti ya Mungu.
Ndugu zangu nafahamu kazi iliyoko mbele yangu ni ngumu, lakini kwa pamoja tunaweza, hivyo nawaomba ushirikiano wenu wa hali na mali,” alisema. Alisema kilichomsukuma zaidi ni kutokana na hali ya Watanzania kukandamizwa kwa muda mrefu na sera mbovu za CCM kwa kipindi cha miaka karibu 50, huku wakiporwa haki yao ya msingi kukosekana kwa utawala bora na utawala wa sheria .
Akizungumzia mrithi wake wa Jimbo la Karatu, Dk.Slaa aliwatoa hofu wananchi waliokusanyika katika mkutano huo kuwa atapatikana mgombea makini ambaye atafanyiwa utafiti wa kutosha kabla ya jina lake kuwasilishwa kwa wananchi na jimbo hilo litaendelea kubakia mikononi mwa chama hicho. Wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ya kumrithi Dk.Slaa ni pamoja na aliyepata kuwa Mkurugenzi wa Mradi wa Maji wa Bonde la Pangani (Pangani Water Basin Project) ambaye kwa sasa amestaafu Julius Sarmet, Petro Paul Ahham, ambaye ni Mkurugenzi wa Shirika lisilo la Kiserikali (NGO) la Messo; Titus Lazaro Massay ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Karatu na Illy Qambalo ambaye ni Mratibu wa Miradi wa Jimbo Katoliki la Mbulu.
Hata hivyo, habari za ndani ya chama hicho ngazi ya wilaya zilieleza kuwa mchakato wa kupata jina la mgombea mmoja uliokuwa ukifanywa na kamati maalumu ulishindwa kufikia muafaka baada ya baadhi ya viongozi wa wilaya hiyo kutaka kumpitisha Mwenyekiti wa Halmashauri Titus Lazaro Massay lakini baadaye mpango huo ulipingwa na baadhi ya wajumbe. Hata hivyo, kati ya wagombea hao, Qambalo ndiye aliyekuwa akipewa nafasi kubwa lakini inaelezwa kuwa mgombea huyo alikuwa amechukua fomu za kuwania ubunge kupitia CCM, akazibwaga dakika za mwisho kitendo kinachoelezwa ya kuwa kinaweza kumwondolea sifa ya kuteuliwa na CHADEMA.
“ Tumeonelea tuwasubiri viongozi wa ngazi ya Taifa kwa mashauriano zaidi ili kupata mgombea wa uhakika ambaye atauzika kwa wananchi kwa urahisi zaidi na ambaye pia atafuata nyayo za Dk.Slaa,” alisema mmoja wa viongozi wa ngazi ya wilaya aliyeomba jina lake lihifadhiwe. Kwa upande wa CCM hapa, ambacho kimekuwa chama cha upinzani katika Jimbo la Karatu kwa miaka 15 sasa, viongozi wake wanadaiwa kuwa wamefadhaishwa na mapokezi makubwa aliyopata Dk.Slaa na matumaini yao ya kunyakua kiti cha ubunge yametiwa shaka na kushamiri kwa makundi ndani ya chama hicho kwa muda mrefu. ends.
