MIMI sio mpenzi wa mchezo wa kamari lakini mwaka 2002 nilijishindia Shilingi 5,000 za bure kutoka kwa rafiki yangu wa karibu kutokana na kushinda ubishi uliohusu uchaguzi mkuu uliokuwa ukifanyika nchi jirani ya Kenya.
Ilivyokuwa ni kwamba Desemba, mwaka huo wa 2002, Kenya ilikuwa inafanya uchaguzi mkuu uliokuwa na upinzani mkubwa kati ya chama tawala cha KANU na Umoja wa Vyama vya Upinzani nchini humo uliofahamika kwa jina la National Rainbow Coalition.
Chama tawala cha KANU kilikuwa kimemsimamisha kama mgombea wake wa uraisi Uhuru Kenyatta ambaye alikuwa ameandaliwa na raisi aliyekuwa anaondoka madarakani, Daniel Arap Moi kuwa mrithi wake; huku National Rainbow Coalition kikiwa kimemsimamisha Emilio Mwai Kibaki kama mgombea wake.
Rafiki yangu huyo ambaye ni kada mzuri wa chama tawala nchini (CCM) lakini si mfuatiliaji mzuri wa masuala ya siasa yasiyohusu chama chake, alikuwa akisisitiza kuwa hakukuwa na namna yoyote ambapo chama tawala cha KANU, chini ya mgombea wake Uhuru Kenyatta, kingeondolewa madarakani.
Juhudi zangu za kumfahamisha kuwa, kwa mujibu wa vyanzo vingi vya habari vya nchini Kenya; hususani magazeti, kama ilivyokuwa kwa mfalme Nebuchadnezzar, maandishi yalikuwa tayari ukutani kwa chama tawala cha KANU; hata kama chenyewe kilikuwa kinajitia kutoyaelewa, zikagonga ukuta.
Tukaishia kuwekeana dau la Shilingi 5,000 (zilikuwa nyingi wakati huo!) kwa ambaye utabiri wake ungekuwa sawa.
Kilichotokea ni historia. National Rainbow Coalition na Mwai Kibaki kikaibwaga vibaya KANU iliyokuwa madarakani na Uhuru Kenyatta wake kwa zaidi ya nusu ya kura zilizopigwa. Mwai Kibaki akipata asilimia 61.3 ya kura zilizopigwa huku Uhuru Kenyatta na chama tawala wakiambulia asilimia 20.2 na kuthibitisha kuwa hakuna kisichowezekana chini ya anga.
Zilitolewa sababu kadha wa kadha kuhusu chama tawala cha KANU kubwagwa vibaya kwenye uchaguzi ule ikiwemo kosa la raisi Daniel Arap Moi kushinikiza Uhuru Kenyatta kutoka familia yenye nguvu ya raisi wa kwanza wa nchi hiyo, Jomo Kenyatta, kuwa mgombea uraisi wa KANU pamoja na kutokuwa mzoefu wa mikiki mikiki ya kisiasa. Iwavyo vyovyote, Shilingi 5,000 za rafiki yangu zikawa historia kwake.
Nimeyakumbuka haya baada ya kusikiliza kauli mbali mbali za kujikatisha tamaa kutoka kwa wanasiasa na wananchi wa kawaida nchini kuhusu uamuzi wa CHADEMA kumsimamisha Dk. Wilbroad Slaa kuwa mgombea nafasi ya uraisi kutoka chama hicho kwenye Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka huu.
Miongoni mwa kauli zilizoshangaza ni ile iliyotolewa na aliyekuwa kiongozi wa kambi ya Upinzani bungeni, Hamad Rashid Mohamed ambaye alinukuliwa na gazeti moja nchini akisema kuwa hatua ya Dk. Slaa kuwania uraisi ni pigo kwa Upinzani; kwani michango muhimu na changamoto alizotoa bungeni zitakosekana.
Huyu ni kiongozi wa kambi ya Upinzani bungeni ambayo moja ya malengo yake makubwa ni kuiondoa Serikali ya CCM madarakani kupitia sanduku la kura. Ili kufikia lengo hili, wapinzania wanategemewa kutumia ‘silaha’ zao zote halali walizo nazo.
Katika kipindi cha miaka 15 alichokaa bungeni Dk. Slaa amejibainisha kuwa ni silaha muhimu katika mikakati ya vyama vya upinzani wa kuikosoa na hatimaye kuiondoa madarakani serikali.
Nilidhani kwamba kiongozi wa kambi ya Upinzani ndio angekuwa mtu wa kwanza kabisa kumpongeza Dk. Slaa kwa hatua yake ya kutafuta nafasi ya kutumikia taifa baada ya kutumikia jimbo lake kwa mafanikio.
Inashangaza pia matamshi ya kiongozi huyo wa Upinzani yanapoelekea kutuaminisha kuwa miongoni mwa wabunge wengi wa Upinzani tunaotegema wataingia bungeni, hakutakuwa na mbunge atakayeweza kuitingisha serikali kwa changamoto na michango muhimu na kufanya pengo la Dk. Slaa lisionekane.
Zipo pia taarifa za kusikitisha za baadhi ya wananchi kudai kuwa Dk. Slaa anafaa zaidi kuendelea kukaa bungeni badala kugombea uraisi kwa vile akishindwa bunge litakuwa limepoteza mtu muhimu ambaye aliweza kutoa changamoto zilizoitingisha serikali.
Upeo wa mambo wa watu wenye aina hii ya mtazamo unatia wasiwasi. Hivi watu hawa wangependa Dk. Slaa akae bungeni kwa miaka mingapi ndipo waamini kuwa sasa anafaa kuwa mgombea uraisi? Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere alipoanza kuiongoza nchi hii aliishakaa bungeni miaka mingapi ili kupata uzoefu?
Lakini pia kwa wale wanaodai kuwa Dk. Slaa hajafanya maandalizi ya kutosha kuwa raisi, mbona wapo viongozi ambao tunaambiwa kuwa walifanya maandalizi ya kuwa viongozi kwa miaka kumi lakini mwisho wa yote ‘marejesho’ ya maandalizi hayo hayalingani na muda mrefu wa maandalizi uliotumika?
Lakini swali kubwa kuliko yote tunalopaswa kujiuliza ni lile la kwamba ni kitu gani kinachowafanya watu hawa kuamini kuwa Dk. Slaa atashindwa? Wamesahau yaliyotokea kwenye uchaguzi mkuu wa Kenya wa mwaka 2002 ama ule wa Marekani wa mwaka jana?
Kama hayo yaliweza kutokea huko, kwa nini yasiweze kutokea hapa?
Tukichukua na kuyatafakari maneno ya baba wa taifa kuwa ‘Ikulu ni Mzigo na watu safi kabisa hawapakimbilii’, tunadhani kuwa Dk. Slaa anastahili kabisa kuwa mgombea wa urais mwaka huu. Hajapakimbilia. Hajatuambia kuwa ‘ametumwa na wazee’ ama ‘wazee wamemuomba’.
Amekubali kuingia kwenye mchakato wa kugombea urais baada ya kushauriwa kufanya hivyo na Watanzania wanaoitakia mema nchi yetu.
Wapo watu ambao kwa zaidi ya miaka kumi na tano sasa, maneno ya ‘uchaguzi mkuu’ na ‘kuteuliwa kugombea urais’ yamekuwa kama majina yao ya katikati.
Kwa hakika, ndani ya vyama vyao unapotamka maneno hayo ni kama umewaita na haiyumkini wakaitikia kwa sauti!
Ninaamini kuwa ni jambo jema kwa demokrasia yetu changa kwa Dk. Slaa kugombea nafasi ya uraisi. Itakuwa ni jambo jema pia iwapo Profesa Ibrahimu Lipumba atashauriwa na akakubali kujitoa kwenye mbio za kugombea urais mwaka huu na kuunganisha nguvu zake, za CHADEMA na vyama vingine vya upinzani kumuunga mkono Dk. Slaa.
Uzoefu ambao Profesa Lipumba ameupata katika mara tatu alizojaribu kugombea urais na kushindwa, vitamsaidia sana Dk. Slaa. Huu ni mwaka ambao wapinzani wanapaswa kuweka ubinafsi kando na kukubali kumsimamisha Dk. Slaa kuwa mgombea uraisi pekee kutoka Upinzani ili kutoa upinzani wa kweli kwa chama tawala.
Watanzania sasa wako tayari kwa mabadiliko. Kwa hakika, sio jambo jema kwa nchi zetu changa hizi kidemokrasia mgombea urais kutoka chama tawala kushinda urais kirahiisi kama anasukuma mlevi vile kila baada ya miaka mitano.
Ni lazima aonje joto ya jiwe kwenye harakati zake za kuutafuta urais ili hata pale anapoupata auheshimu kwa vile ameutolea jasho.
Tunategemea pia taasisi za habari nchini zitaandaa midahalo baina ya wagombea urais ili wapiga kura tupate nafasi ya kupembua mchele na pumba, kama ilivyo kwa nchi nyingine. Tunategemea pia taasisi hizi zitajitahisi kuhakikisha kuwa hakuna mgombea atakayeingia mitini.
Tunataka rais anaposhinda urais aonekane kweli amefanya kazi ili kuupata. Rais wa nchi anaposhinda urais kwa kuwaburuza wagombea urais kutoka vyama vya Upinzani ambao kwa nchi yetu ni wale wale kwa miaka kumi na tano iliyopita, demokrasia yetu inaishia kuonekana kama mchezo wa kuigiza.
Ni wazi kwamba upinzani wa kweli kama anaotegemewa kuutoa Dk. Slaa utakifanya chama tawala ku- sit up and take note, chambilecho Baba wa taifa.
Na hili litaanzia kwenye kwenye kampeni za urais.
Chama tawala sasa kitalazimika kupanga mikakati mipya ya kukabiliana na mgombea urais mpya kutoka Upinzani tofauti na ambavyo wangefanya kwa wagombea waliowazoea ambao hata hawawakoseshi usingizi tena.
Kutokana na hili, chama tawala kitalazimika pia kuhahakisha kuwa ahadi wanazotoa kwa wananchi ni zile zinazotekelezeka na sio zile ambazo baada ya kuwaingiza madarakani wanaishia kutuambia kirahisi rahisi tu kuwa hazitekelezeki na hakuna anayewajibika.
Kwa hakika, uingiaji wa Dk. Slaa kwenye mchakato wa kugombea urais utafanya baadhi ya vyama ambavyo viliishaandaa fulana 10,000, doti 10,000 za kanga na gunia 10 za mchele kwa ajili ya pilau la kuwahadaa wananchi kuvipigia kura, sasa vitalazimika kuandaa fulana 20,000, doti 20,000 za kanga na gunia 20 za mchele ili kukabiliana na kimbunga cha Dk. Slaa!
Hii itasaidia angalau wananchi wetu wengi zaidi; hususani huko vijijini kwetu ambao hukumbukwa zaidi nyakati hizi, kuambulia fulana na doti za kanga lakini wanaposimama peke yao mbele ya sanduku la kura wanajua ni nani wa kumpa kura zao. Hakika, Dk. Slaa katika uchaguzi wa safari hii atawaamsha hata waliolala kwa kukata tamaa!

Blogu: