SEHEMU nyingi nchini mtu anayeshona nguo ama mpya au kuweka viraka katika nguo za zamani, anaitwa fundi cherehani. Ulipata kujiuliza kwa nini waliitwa fundi cherehani?
Utaalamu wa watu hao ni kusanifu na kushona nguo au kuweka viraka. Nilidhani fundi cherehani ni yule mwenye ujuzi au utaalamu wa kuzifanyia matengenezo mashine tunazoita cherehani!
Watunga mashairi wangeweza kulijadili swali hilo vizuri. Washairi huwa wana kipaji cha hali ya juu ikiwemo uwezo wa kuuliza swali na kulijibu vyema; ingawa wakati mwingine wanajibu kwa mafumbo; hasa watunga mashairi ya taarabu. Kwa mfano, ewe njiwaaa peleka salamuuu…! hivi ni njiwa yupi huyo?
Baada ya mchapo huo mdogo, turudi kujadili mada ya leo inayoangalia madini ya vito ya tanzanite kuwa huenda, kwa Tanzania, ni fursa iliyopotea.
Kabla hatujaendelea, ipo haja tuwe pamoja kuhusu tahadhari inayohusiana na masuala ya rekodi. Nchini petu masuala mengi hayana rekodi au kumbukumbu iliyoandikwa na kutunzwa vizuri ambapo mtafiti anaweza kurejea bila tatizo.
Masuala mengi ya nchi yetu tunayapata kwenye masimulizi. Rafiki yangu mmoja, Bwana Majjid Mjengwa, hivi karibuni, aliandika katika gazeti hili la Raia Mwema kuwa: “Wengi tunasimuliwa na hata kusimulia hadithi za sungura mjanja”.
Tafsiri fupi ni kuwa hata hizi hadithi za sungura mjanja ambazo makabila mengi ya Tanzania wanazisimulia, hazijaandikwa ila zipo katika masimulizi ya bibi au babu na wajukuu zake.
Elimu yetu huko baadaye ikiwa itahimiza wanafunzi kufanya utafiti na kuhoji mausala na kuacha utamaduni wa “ndiyo mzee” au “ndiyo bosi”, kama ilivyo sasa , kizazi hicho kitapata tabu kufanya rejea.
Suala unalotafiti kama halina rejea za kutosha utafiti unakuwa wa mashaka mashaka. Utafiti wenye tija ni ule ambapo unaangalia wenzako walifanya nini na wewe unataka uongezee nini kwenye hilo suala.
Bahati mbaya, nadhani wengi wetu hatujui kama nchini tunayo sera ya utafiti. Nchi, hasa zile zilizoendelea na zinazotaka kuendelea kwa msingi wa maaendeleo ya nchi kweli kweli, utafiti ni sera kuu na hutumia sehemu kubwa ya Pato la Taifa.
Hapa nchini kwetu, wengi hatujui ni asimilia ngapi ya Pato la Taifa inatumika kwenye nyanja ya utafiti. Hoja hii inaweza kuwa mjadala mkubwa hivyo tuiachie hapo na tuendelee na mada ya leo ya tanzanite.
Tanzanite ni madini ya vito yanayopatikana sehemu moja tu duniani. Sehemu hiyo ni Mirerani (wengine wanaita eneo hilo Merelani), wilayani Simanjiro, Mkoa wa Manyara.
Inawezekana huko baadaye madini haya yakapatikana sehemu nyingine Tanzania au sehemu nyingine duniani.
Madini mengi duniani, kwanza yalianza kugunduliwa eneo moja. Baada ya watu kujua matumizi, umuhimu wake na uhitajika wake kwa binadamu, utafiti ulifanyika kwa bidii na kubahatika kuyagundua sehemu nyingine. Hivyo tanzanite kuweza kupatikana sehemu ingine Tanzania au kwingine kokote duniani, haitakuwa ajabu.
Sasa turejee kutumia neno tuliloanza nalo la fundi cherehani.
Inasemekana jiwe ambalo baadaye lilikuja kujulikana kama madini ya vito ya tanzanite liligundulika mnamo mwaka 1966 na mfugaji wa eneo la Mirerani aliyejulikana kwa jina la Ali Juuyawatu.
Aidha, inasemekana Bwana Juuyawatu, kwa kushangazwa na mng’aro wa jiwe alilookota hapo Mirerani, alilipeleka kwa fundi cherehani mmoja ambaye pia alikuwa anafahamika kuwa alijihusisha na utafiti na ununuzi wa madini ya vito vya bluu ambavyo kwa lugha ya kitaalamu vinaitwa blue sapphire.
Fundi cherehani huyo alijulikana kwa jina la Bwana Manuel D’Souza na aliishi na kufanya shughuli zake za kushona nguo na kununua madini ya vito mjini Arusha.
Nyaraka nyingi zilizochapishwa katika majalada mengi sehemu mbalimbali duniani zinataja ugunduzi wa tanzanite kwa kumhusisha Ali Juuyawatu na Bw. D Souza. Hakuna aliyewahi kukanusha au kudhibitisha uhusiano huo. Si Serikali ya Tanzania wala si chombo chochote cha utafiti nchini kilichopinga taarifa au madai hayo.
Mashaka yanaanzia hapo. Kwamba miaka ile ya 1960 eneo lile la Mirerani ambalo ni la wafugaji, hasa wa kabila la Wamaasai, kulikuwa na Mmasai anaitwa Ali Juuyawatu!? Wamasai wengi, kama si wote, tunawajua kwa manajina ya ukoo yanayoanzia na Ole. Kwa mfano; Ole Naiko, Ole Sendeka, na kadhalika na kadhalika.
Ndiyo, ni kweli wapo wachache kama vile Edward Lowassa hawana Ole, lakini jina la Ali Juuyawatu linatia mashaka kiasi fulani.
Ili kutopanua mjadala wa mada ya leo, hoja ya Ali Juuyawatu inaishia hapo. Kuendeleza mjadala huo ni sawa na uibuaji wa hoja kama vile; ni kwa nini baadhi ya machapisho sehemu nyingi duniani yanaonyesha Mlima Kilimanjaro upo nchini Kenya!
Tuendelee na hoja ya kuwa kwa nini tanzanite inaweza kuwa ni fursa iliyopotea. Inasemekana ni Bw. D’Souza ndiye aliyepeleka jiwe hilo kwa wataalamu wa kutambua madini.
Hatimaye kampuni maarufu ya Marekani inayoitwa Tiffany, inayouza vidani nchini Marekani na sehemu nyingi duniani, ilipata madini hayo na kuyachunguza kimaabara ili kujua ni madini ya aina gani?
Kampuni hiyo ya Tiffany, baada ya kuyafanyia uchunguzi wa kimaabara walibaini kuwa madini yale ni madini ya vito ambayo hayajawahi kungundulika kwingine kokote duniani na kwa heshima ya nchi yalipogundulika wakayaita tanzanite.
Kutokana na mng’aro wake wa bluu unaowakawaka; hasa baada ya kuchongwa kwa mtindo, kampuni ya Tiffany ilihamasisha matumizi yake katika vidani nchini Marekani.
Inasemekana madini hayo yalipata umaarufu na kupendwa kwa muda mfupi, kuliko madini mengi ya vito yalivyowahi kupata umaarufu.
Zipo taarifa ambazo hazijabithitishwa au kukataliwa kuwa Tiffany, baada ya kuona fursa kubwa ya kupata biashara kwa kutumia madini hayo mapya, ilikuja Tanzania na kutaka kununua au kumilikishwa eneo ambalo tanzanite ilikuwa inachimbwa wakati huo; hasa na wachimbaji wadogo wakiongozwa na Bw. D’Souza.
Lakini kama tunavyojua, miaka ile ya mwishoni mwa 1960 ilikuwa ni miaka ya vugu vugu la Azimio la Arusha ambalo halikuwa na mwanya wa ukiritimba wa mtu mmoja mmoja au kampuni moja ambayo si ya umma kuhodhi mali ya umma.
Inawezekana, kwa sababu hiyo, walishindwa kuhitimisha matamanio yao ya kuhodhi uzalishaji na usambazaji wa tanzanite, wakati huo.
Hatuhusishi na kudhania kwetu kuwa tanzanite ni fursa iliyopotea na madai ya kampuni ya Tiffany kushindwa kuuziwa au kumiliki uzalishaji wa tanzanite miaka hiyo; tendo ambalo lingewafanya kuhodhi na kuwa na ukiritiba mkubwa wa tanzanite kote duniani.
Fikra kuwa huenda tanzanite ni fursa iliyopotea tunaihusisha na mkakati ambao hutumiwa; hasa katika bidhaa ya madini ya vito. Tutaeleza baadaye mkakati huo ulivyotumiwa ipasavyo katika madini ya vito ya aina ya almasi duniani.
Zipo sifa kadhaa zinazofanya vito vipendwe na kuuzika kwa bei nzuri katika masoko ya kimataifa. Sifa mojawapo kubwa ni upatikanaji wake kuwa haba na adimu. Kwa lugha ya kitaalamu ya wajemolojia (gemologist) wanaita uadimifu (rarity).
Tanzanite hadi tunapoandika makala hii inapatikana na kuchimbwa sehemu moja tu duniani; yaani Mirerani nchini Tanzania. Kupatikana sehemu moja kunaifanya tanzanite kuwa adimu sana kuliko almasi inayochimbwa mabara yote duniani.
Hakuna bara ambalo almasi haichimbwi! Kwa Bara la Afrika almasi inachimbwa na nchi nyingi; kwa mfano, Angola, Afrika Kusini, Botswana, DRC, Liberia, Namibia, na Tanzania.
Moja ya mkakati uliotumiwa na kampuni iliyoanza kuhodhi ukiritimba wa almasi tangu miaka ya 1850 - kampuni ya De Beers ya Afrika Kusini, ni kufanya madini hayo yaonekane adimu sana.
Kwanza, kwa De Beers kujihusisha na kumiliki migodi au kununua almasi nyingi zilizochimbwa katika nchi mbalimbali duniani. Pili, kwa kuzipa almasi madaraja mbalimbali na daraja la juu kabisa kulifanya ni adimu sana.
De Beers walitumia mkakati huo wa kuhodhi na ukiritimba kuwawezesha kuathiri au kushawishi almasi ziuzwe kwa bei kubwa kuliko wangeacha soko liwe la ushindani!
Mkakati huo wa De Beers umefanya kazi kwa zaidi ya miaka 100. Hata hivyo, miaka ya hivi karibuni ukiritimba huo umepunguzwa nguvu; hasa kwa sababu ya Sheria za Marekani na Uingereza za anti-trust, na Nchi Zilizoendelea, kama vile Australia na Kanada, kugundua migodi yao ya almasi na kutokukubali kuuza almasi zao kupitia mtandao wa De Beers.
Hoja yangu ni kwamba, kwa kuzingatia uadimu wa tanzanite, tungeweza kutumia mkakati kama huo wa De Beers; lakini kwa kuzingatia mazingira yetu kujiletea mapato makubwa zaidi.
Kwa sasa uendeshaji wa biashara ya tanzanite, ni wa kiholela tu bila mkakati. Jibu la uholela huu ni kuwa hatupaswi kuingilia soko huria. Ukiendeleza mjadala kama huo, utapata majibu ya kuwa tunapaswa kuheshimu mikataba ya kimataifa ambayo tumo (kama vile World Trade Organization - WTO) inayozuia ukiritimba wa kibiashara.
Lakini, wengine walio na maliasili za mafuta wana ukiritimba (mfano OPEC); licha ya uwepo wa WTO. China nayo mara nyingi wanasema kuwa hawapaswi kuingiliwa na mataifa mengine kuhusu mbinu zao walizojichagulia kujiletea maendeleo; maana hiyo ni sawa na kuingilia uhuru wa nchi yao.
Aidha, tanzanite pia ingeweza kutoa ajira kwa vijana kuliko ilivyo sasa; hasa kama utaratibu ungekuwepo wa kuzuia madini hayo kusafirishwa bila kusanifiwa na kuchongwa hapa hapa nchini.
Tatizo ni hoja inayojengwa kwamba hakuna wasanifu, wakataji na wachongaji wa kutosha wa vito nchini! Lakini; kwa nini wanaohitaji tanzanite isiyokatwa na kuikata kwao, wasiambiwe waje wawekeze shughuli hiyo ya kukata hapa nchini mwetu?
Botswana wamefanikiwa kwa hili la kuwataka wanaohitaji almasi zao wafungue viwanda vya kusanifu, kukata, na kuchonga almasi nchini Botswana. Kwa nini sisi tushindwe kuwaiga Botswana? Kinachotakiwa ni uamuzi tu.
Katika Bunge la Bajeti la mwaka 2003/2004, waziri mhusika wa sekta ya madini alitangaza kuwa utaratibu utawekwa ili kuzuia tanzanite (nadhani za kuanzia uzito wa gramu mbili) kutosafirishwa nje bila kukatwa nchini.
Kufuatia taarifa ile ya Bungeni, India (moja ya nchi marafiki wetu) ambapo ndipo tanzanite nyingi; hasa zile ndogo ndogo zinapokatwa, ililalamika kuwa watu wao watakosa kazi ikiwa uamuzi huo utatekelezwa. Baada ya lalamiko hilo la India utekelezaji wa sera hiyo (waziri anapotamka suala Bungeni hiyo ni sera), haukufanyika!
Suala la nchi marafiki kufuatilia sera zetu na kutuingilia na sisi kukubali, pia tunaliona wakati wa kupitia na kujadili mikataba ya madini. Wakati wa kujadili mikataba ya madini Kanada na Uingereza walifuatilia sana na kutuaminisha kuwa tunayumba; huku wakitusifu eti sera tulizonazo zimewezesha uwekezaji wa hali ya juu kwenye sekta ya madini!
Kufuatia ufuatiliaji wa wakubwa hao (Canada na Uingereza) sote tunajua nini kilipatikana katika mijadala ile ya mikataba ya madini! Si nia ya makala hii kuleta mjadala mwingine mrefu wa jinsi tunavyosalimu amri kwa nchi tajiri zinazotusaidia kuziba naksi kubwa ya Bajeti ya Serikali.
Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, aliwahi kusema kuwa wakubwa wakisema (yaani, nchi tajiri kama Marekani) inabidi usikilize na kuwaendea pole pole.
Tuishie hapa kwa leo; kwa ujumbe kwamba Mwenyenzi Mungu akikutunuku uwezo ambao hakuwapa wengine, uutumie vyema kutatua matatizo ya watu wako na usijali kwamba unahitajika kuonekana unatekeleza matakwa ya soko huria.
Tafakari.
