BAADA ya CHADEMA kumtangaza Dk.Slaa kuwa mgombea urais kupitia chama hicho, kuna uwezekano mkubwa majimbo sita ya uchaguzi mkoani Kagera kwenda Upinzani. Majimbo hayo ni Karagwe, Biharamulo, Bukoba Mjini, Ngara, Muleba Kaskazini na Bukoba Vijijini.
Ni imani yangu pia kwamba hata mikoa mingine majimbo mengi yataangukia mikononi mwa wapinzani kutokana na ushawishi mkubwa wa Dk.Slaa.
Inawezekana Dk.Slaa akashindwa kumwangusha Rais Kikwete katika uchaguzi mkuu; maana sheria yetu ya uchaguzi inamruhusu mwenye kura nyingi kuwa mshindi; hata kama kura zenyewe hazifikii nusu, lakini ni wazi Upinzani utakuwa umepata viti vingi, kitu kinachoweza kuchangia mabadiliko makubwa katika taifa letu yatakayoharakisha maendeleo.
Na hiki ndicho tunachokihitaji; maana chama kimoja hakiwezi kuleta maendeleo na chama kimoja hakitoi picha ya demokrasia tunayoiimba na kuikumbatia katika katiba yetu.
Siandiki makala hii kwa kuwa nina chuki na chama fulani cha siasa au nina chuki binafsi na mgombea yeyote yule. Ninaandika kwa kusoma alama za nyakati na kusukumwa na hitaji la nyakati tulizomo. Taifa letu linahitaji mabadiliko chanya ya kutusaidia kuleta maendeleo kwa Watanzania wote.
Kujifanya tunalipenda taifa letu wakati tunayashughulikia matumbo yetu, familia zetu, ndugu zetu, marafiki zetu na kulitelekeza taifa zima ni dhambi isiyokuwa na msamaha!
Mawazo kwamba kuna Watanzania wenye haki ya kuishi na kufurahia matunda ya taifa hili zaidi ya wengine, pia ni dhambi kubwa isiyokuwa na msamaha. Tanzania ni yetu sote, ni wajibu wetu sote kuipenda, kuilinda na kuitumikia kwa nguvu zetu zote.
Kama baada ya hotuba ya Rais Kikwete ya kulivunja Bunge tungeingia kwenye uchaguzi mkuu, ni wazi CCM ingepata kura nyingi na kujizolea majimbo mengi kwa kishindo. Lakini kitendo cha CHADEMA kukubali kumsimamisha Dk.Slaa kimeleta changamoto kubwa na kubadilisha upepo.
CCM haiwezi tena kushinda kwa kishindo kama uchaguzi utakuwa huru na wa haki. Alama za nyakati zinaendelea kuonyesha kwamba watu wameanza kufumbua macho na kuuona ukweli.
Mchambuzi aliye makini ni lazima agundue kwamba hata ndani ya CCM mambo si shwari. Kumpitisha Kikwete bila kupingwa haina maana makundi na mivutano vimekwisha. Kuna wana CCM wana machungu ya ndani lakini wanaogopa kujitokeza. Hawa ‘watajitokeza’ kimya kimya ndani ya chumba cha kura ambako hakuna uwezekano wa kujua nani kampigia nani.
Kwa vile Dk. Slaa ni mtu makini, mzalendo, msomi, mcha Mungu na mpenda maendeleo, kuna uwezekano hata wana CCM wenye machungu ndani ya chama chao wasiofurahi jinsi mambo yanavyokwenda, wakampigia kura Dk.Slaa pamoja na wagombea wengine atakaowanadi.
Ni bahati mbaya kwamba tunaingia kwenye uchaguzi bila tume huru ya uchaguzi, na bila ya kuwa na wagombea huru. Tungekuwa na tume huru na wagombea huru ningesema kwa asilimia 100 kwamba majimbo sita ya uchaguzi mkoa wa Kagera yatakuwa mikononi mwa Upinzani; kwa maana kwamba mgombea wa CCM asingeweza kushinda katika majimbo haya.
Sasa kwa vile tume ni ile ile iliyochaguliwa na Serikali iliyo madarakani na kwa asilimia kubwa inahakikisha inaitumikia serikali hiyo ya CCM, ni vigumu kusema kwa uhakika lakini dalili zote zinaonyesha Upinzani kuweza kuyateka majimbo hayo sita katika mkoa wa Kagera.
Watu wakiamua kuzilinda kura zao wenyewe na kuhakikisha hakuna udanganyifu katika kuhesabu na kujumlisha kura, matokeo yanaweza kuwa mazuri kwa pande zote; wapinzani na Chama tawala. Haki inaweza kutendeka bila kulazimika kufanya kama walivyofanya kule Kenya.
Halitakuwa jambo jipya baadhi ya majimbo ya mkoa wa Kagera kwenda Upinzani. Tofauti ni kwamba zamu hii yatakuwa mengi. Jimbo la Kyerwa, Biharamulo, Muleba Kaskazini na Bukoba mjini, yalishaanguka mikononi mwa wapinzani na baadaye “kukombolewa”. Yote yaliyokombolewa isipokuwa Kyerwa, yako hatarini tena kurudi Upinzani na kuongezea mengine.
Kyerwa itapona kwa vile mbunge aliyemaliza muda wake, Bwana Katagila ana nafasi kubwa ya kushinda kura za maoni za CCM baada ya wagombea wawili wanaokubalika kiasi fulani kujitokeza kumpinga Bwana Katagila. Kuna uwezekano mkubwa mabwana hawa wawili kugawana kura na Bwana Katagila akapeta.
Hata hivyo, mchango wa Bwana Katagila katika miradi ya maendeleo ndani ya jimbo lake, ni mkubwa. Kampuni yake ya Kahawa inatoa mchango mkubwa kwa kununua kahawa kwa bei ya juu na kuhakikisha wakulima wanapata fedha zao kwa wakati, amehamasisha ujenzi wa mashule na sasa anajenga chuo cha walimu katika jimbo lake la uchaguzi.
Watu wanaamini ni yeye aliyepambana hadi Jimbo la Kyerwa likawa wilaya.
Jimbo la Karagwe linaweza kwenda Upinzani. Kama tulivyosema kwenye taarifa ya wiki iliyopita, mchuano mkali kwenye kura za maoni za CCM ni kati ya Karim, Blandes na Profesa Ngalinda. Wote watatu wana nafasi ya kuchaguliwa. Blandes ni mbunge anayemaliza muda wake, ni wazi ana nafasi nzuri ndani ya uongozi wa CCM kuanzia wilayani, mkoani hadi taifa.
Karim ni mchumi wa CCM wa wilaya. Nafasi hiyo inamfanya awe na nafasi nzuri ndani ya uongozi wa CCM wilayani, mkoani hadi taifa. Profesa Ngalinda naye amekuwa msaada mkubwa kwa Chama tokea wilayani hadi taifa. Hata hivyo, wote watatu hakuna mwenye ubavu wa kupambana na moto atakaouwasha Dk.Slaa.
Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe iko ndani ya kashfa kubwa na baadhi ya watendaji wake, akiwemo Mkurugenzi wa Halmashauri, wamesimamishwa kazi. Tuhuma zilizotolewa ni pamoja na uuzaji wa zabuni hewa na wakandarasi wasiokuwa na sifa (ubovu wa barabara), mishahara ya watumishi waliokufa na kufukuzwa kutumiwa vibaya, uwanja wa michezo (mpira) unaodaiwa kutengenezwa kwa milioni 104 wakati haujaisha, watumishi 14 kesi yao iko mahakamani kwa tuhuma za kughushi zaidi ya Sh.milioni 46, kutumia madaraka vibaya, zabuni hewa za vyakula vya wanafunzi na mengine mengi.
Wananchi wanasubiri majibu ya tuhuma hizi na hatua zitakazochukuliwa. Sioni Serikali kufanikiwa kuyaweka sawa mambo hayo kabla ya uchaguzi mkuu.
Sote tunafahamu kwamba pamoja na Dk.Slaa kuibua maswala ya ufisadi, rushwa na sheria zinazopitishwa bila umakini, amekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Serikali za Mitaa. Anajua madudu yote yanayotendwa kwenye serikali za mitaa. Ana takwimu zote na mifano iliyo hai.
Akisimama Karagwe kumnadi mgombea wa CHADEMA na kuonyesha jinsi CCM ilivyoshindwa kuiendesha Halmashauri ya Karagwe, itakuwa ajabu kwa mgombea wa CCM kushinda.
Tatizo la Karagwe linaweza kufanana na Bukoba Mjini. Ingawa CCM imempitisha Balozi Kagasheki bila kupingwa, na kwa kiasi sasa hivi Balozi Kagasheki anakubalika zaidi kama ilivyokuwa uchaguzi mkuu wa 2005, bado kuna hatari ya Dk. Slaa kumnadi Bwana Lwakatare kwa nguvu zote kwa kutumia udhaifu wa utendaji wa Manispaa ya Bukoba Mjini.
Michango ya Balozi Kagasheki anayoitoa katika jimbo lake la uchaguzi, anaitoa yeye kama Kagasheki na si kama Manispaa. Wananchi wangependa kuona utendaji mzuri wa Manispaa yao.
Kwa vile Balozi Kagasheki ni waziri, hakupata nafasi ya kutosha kujikita kwenye masuala ya chini yanayowagusa wapiga kura wake. Pia Lwakatare bado anapendwa na anakubalika Bukoba Mjini. Nguvu zake, nguvu za wananchi, nguvu za wanachama wa CHADEMA na nguvu za Dk.Slaa zikiungana, kuna uwezekano mkubwa jimbo la Bukoba Mjini kuwa mikononi mwa Upinzani.
Kosa litakalofanyika Bukoba Vijijini ni kumrudisha Bwana Karamagi kama mgombea wa CCM. Ingawa wagombea wa CCM wanaompinga Karamagi wana ushawishi mkubwa, ni kwamba idadi yao ni kubwa na uwezekano wao kugawana kura na kumpatia Karamagi kuwa miongoni mwa washindi watatu, ni mkubwa.
Na dalili zinaonyesha kwamba jina la Karamagi likipelekwa Dodoma ni lazima litarudi. Kwa kosa hilo, ni lazima ushawishi wa Dk.Slaa umwezeshe mpinzani yeyote atakayejitokeza kugombea Bukoba Vijijini, kushinda.
Kama hoja alizoziibua Dk.Slaa na wenzake Bungeni zilisababisha Karamagi kuachia ngazi ya uwaziri, zitashindwa vipi kumshinikiza Karamagi ‘kuachia’ ngazi ya ubunge?
Marehemu Balozi Ngaiza aliacha amejenga mtandao wa CHADEMA kule Muleba Kaskazini. Hata CCM ikimrudisha Ruth Msafiri kugombea, hakuna uwezekano wa kupambana na Dk. Slaa, akiwa anamnadi mgombea wa Upinzani katika jimbo hilo.
Biharamulo tulishuhudia jinsi CHADEMA ilivyopambana na CCM wakati wa uchaguzi mdogo. Wakati ule nguvu zote za CCM zilihamia Biharamulo. Hata na nguvu za dola zilitumika. Utafiti tulioufanya baadaye ulibainisha kwamba wananchi wengi walilalamika jinsi uchaguzi ulivyoendeshwa hadi kutangazwa matokeo.
Wengi wanasema kama si busara za Kabwe Zitto aliyewatuliza wanachama wa CHADEMA na kuwaomba wakubali matokeo, damu ingemwagika na watu wengi wangepoteza maisha yao; maana nguvu za dola zilipita kiasi.
Kama Mukasa atapitishwa na CCM kugombea Biharamulo, ngoma itakuwa nzito. Kwa vyovyote vile upinzani una nafasi kubwa Biharamulo.
Nako Ngara hata kama CCM isipomrudisha Profesa Banyikwa, hakuna mgombea wa CCM mwenye mvuto na ushawishi. Waliojitokeza ni watu wenye majina makubwa kitaifa na kimataifa, lakini hawajatoa mchango mkubwa kule kwao Ngara.
Wafugaji kutoka nchi jirani wamekuwa wakiingiza mifugo yao kwa njia za panya, na serikali imekaa kimya. Kuna ujambazi wa mara kwa mara hadi wananchi wakaamua kujichukulia sheria mkononi. Ngara wamekuwa na kilio cha umeme cha muda mrefu. Ni wazi sasa hivi wangependa kuona mabadiliko. Chama cha NCCR-Mageuzi kina nafasi kubwa ya kushinda katika jimbo hili. La msingi na muhimu ni kumsimamisha mgombea anayekubalika.
Hoja yangu ni kwamba uchaguzi mkuu wa mwaka huu Upinzani una nafasi ya pekee kuonyesha mchango wake katika taifa letu. Mfano Upinzani ukipata majimbo sita kwenye mkoa wa Kagera na kuziongoza Halmashauri hizo, utakuwa mchango mkubwa.
Nina imani Upinzani utapata majimbo mengine kwenye mikoa mingine. Jinsi CCM wanavyoendelea kuchanganyana na kushikana uchawi ndivyo wanavyoupatia Upinzani njia ya kupita.
Ni bora wapinzani kuchangamkia nafasi hii; vinginevyo tutabaki katika mfumo wa chama kimoja cha siasa.

Simu:
0754 633122