TAASISI ya Wahandisi Tanzania imebuni mradi wa kujenga uwezo wa wahandisi wa Tanzania ambao kama utakwenda kama ilivyopangwa, tutaanza kuona kazi tulizozoea zinafanywa na wageni, zikifanywa na Watanzania wenyewe na mwamko wa fani ya uhandisi nchini kuwa mkubwa kuliko ilivyo hivi sasa.
Rais wa taasisi hiyo, Malima Bundara aliwaambia waandishi wa habari jana Jumanne kwamba wamebuni mradi huo kutokana na ukweli kwamba ongezeko la wahandisi wasiokuwa na kazi hata ya kujiajiri inakatisha tamaa vijana kusomea au kujiunga na fani hiyo.
Siyo siri kwamba pamoja na taifa kuzalisha wahandisi wengi kila mwaka, miradi mingi ya maendeleo nchini hufanywa na wahandisi kutoka nje hivyo kugharimu taifa pesa nyingi za kigeni.
Tanzania ina wahandisi waliosajiliwa na Serikali zaidi ya 10,400 na inakadiriwa wahandisi wengine zaidi ya 2,000 hawajasajiliwa kwa sababu mbalimbali.
Wahandisi wanaozalishwa nchini hawatumiki ipasavyo licha ya kuwapo kwa kazi lukuki katika nyanja za nishati na madini, miundombinu, ujenzi wa majumba na mradi wa Kilimo Kwanza.
Kwa mujibu wa Bundara, mradi huo utakuwa ni wa maeneo manne, maeneo hayo yakiwa ni ya uhamasishaji wa shughuli za kiufundi, kurekebisha muundo wa taasisi ili nguvu kazi isiyotumika ya marais wastaafu wa taasisi hiyo ipewe jukumu la ushauri (think tank) ili kutumia uzoefu na utaalam wao. Kukusanya, kuhifadhi na kutumia takwimu za wahandisi mahiri.
Hili suala la kuwa na kumbukumbu au takwimu za wahandisi mahiri nchini ni muhimu mno ili matatizo ya Watanzania yatatuliwe na Watanzania wenyewe kama vile yanapotokea majanga badala ya kuanza kufikiria wahandisi wa nje kwa utatuzi.
Tanzania ina wahandisi ambao ni wataalam wa nyanja mbalimbali lakini kwa vile hakuna kumbukumbu au takwimu zinazowahusu, taifa hulazimika kutumia wahandisi wa nje wenye utalaam ule ule inapotokea shida.
Aidha taifa lisingelazimika kuunda tume za uchunguzi kwa matatiz yanayojikeza kwa vile tume nyingi zimekuwa zikichunguza matatizo ambayo wahandisi wetu wangeweza kuyatatua.
Maoni ya Wasomaji
HIlo ni jambo la msingi
HIlo ni jambo la msingi litatusaidia sisi ambao bado tuko masomoni kujua nini kinachoendelea katika fani ya uhandisi